Ni vigumu kujua aina ya chakula kinachokufaa, bila kujua jinsi mwili
wako unavyokichakata. Kimsingi watafiti wamebaini makundi makuu matatu
ya watu kuhusiana na jinsi miili inavyochakata chakula.
Chakula ambacho ni bora kwa mtu mmoja, kinaweza kuwa sumu baridi kwa mtu
mwingine na kumletea madhara endelevu katika maisha yake. Kwa muktadha
huu basi hakuna chakula bora kwa kila mtu. Chakula ni bora kwa mtu kama
baada ya kukitumia mwili utakipokea vizuri, ukafyonza virutubisho na
kikasaidia kuimarisha afya ya mlaji.
Ni vigumu kujua aina ya chakula kinachokufaa, bila kujua jinsi mwili
wako unavyokichakata. Kimsingi watafiti wamebaini makundi makuu matatu
ya watu kuhusiana na jinsi miili inavyochakata chakula.
Kundi la kwanza ni la wachakataji wa protini. Hawa miili yao
inakubaliana zaidi na vyakula vya protini. Kwa watu wa kundi hili
vyakula vya wanga na hususan vile vilivyochakatwa na kuchujwa kwa
kiwango kikubwa (highly processed and refined), ni sumu baridi ambayo
itawapelekea kuugua maradhi mengi ya kimfumo.
Kundi la pili ni la wachakataji wa wanga. Hawa miili yao inakubaliana
zaidi na vyakula vya wanga. Kwa watu wa kundi hili la vyakula vya
protini, hususan vile vilivyochakatwa na kuhifadhiwa kwa ajili ya kuwa
na muda mrefu wa matumizi, ni sumu baridi ambayo itasababisha kuugua
maradhi mengi ya kimfumo.
Kundi la tatu ni la wachakataji wa vyakula vya protini na wanga kwa
viwango sawa. Kundi hili kidogo lina bahati, kwa maana, halidhuriwi kwa
wepesi na vyakula vilivyoko katika yale makundi mawili ya mwanzo.
Moja ya magonjwa yanayosababishwa na mkanganyiko huu katika kula ni
ugonjwa wa kisukari. Mchakataji wa protini anapokula chakula cha wanga,
kasi ya kuchakata wanga huo ni kubwa mno ikilinganishwa na mlaji
mwenzake ambaye ni mchakataji wa wanga.
Kasi hiyo husababisha kiwango cha sukari kinachoingia katika mzunguko wa
damu ndani ya muda mfupi kuwa kikubwa sana. Kutokana na hali hii
kongosho hulazimika kufanya kazi ya ziada kuzalisha kiwango kikubwa cha
kichocheo kinachojulikana kama insulini ili kuondoa sukari kwenye damu
na kuipeleka kwenye seli ili itumike kutengenezea nishati.
Hali hii ikijirudiarudia, kongosho huchoka na kuanza kufanya kazi chini
ya kiwango au wakati mwingine vipokezi vya sukari katika seli
(receptors) hushindwa kuendana na kasi ya kuletewa sukari kwa ajili ya
matumizi ya seli hivyo huishia kuikataa sukari hiyo.
Hali hii kitaalamu hujulikana kama insulin resistance, au pingamizi
dhidi ya insulini kwa tafsiri isiyo rasmi. Kuna baadhi ya nyakati, vyote
hutokea kwa wakati mmoja, yaani kongosho linafanya kazi chini ya
kiwango, na pia mgonjwa anakabiliwa na pingamizi dhidi ya insulini.
Hivi karibuni imebainika kuwa moja ya sababu kubwa sana zinazosababisha
vipokezi vya seli kushindwa kupokea sukari inayoletwa ni kitu
kinachoitwa mfuro (inflammation). Mfuro ni uvimbe kama lengelenge hivi.
Mfano wa mfuro ni pale unapojikwaa au kujigonga usoni na mwili ukaumuka
na kutengeneza nundu.
Vichocheo vya kusababisha mfuro kwenye seli viko vingi lakini baadhi ya
hivi ni vyakula tunavyokula kila siku. Vyakula hivi ni pamoja na sukari
na wanga uiliochakatwa kwa kiwango kikubwa.
Athari za ugonjwa
Kisukarini ni ugonjwa ambao unasababisha mololongo wa matatizo mengine
ya kiafya mwilini. Matatizo haya ni pamoja na uharibifu wa macho,
unaotambulishwa na magonjwa kama glaucoma ambao husababisha uharibifu wa
neva za jicho.
Matatizo mengine ni ugonjwa ujulikanao cataracts ambao unatokana na
ukungu kwenye lenzi ya jicho na retinopathy unaosababisha uharibifu
katika retina ya jicho.
Matatizo mengine ni ya miguu yanayotambulishwa na magonjwa kama
neurapathy ambayo ni maumivu yatokanayo na uharibifu wa mishipa ya
fahamu, vidonda sugu vya tumbo na gangrene ambao ni mkusanyiko wa tishu
zilizokufa kutokana na kutofikiwa na mzunguko wa damu.
Matatizo mengine ni yale ya magonjwa ya ngozi na magonjwa ya moyo.
Mpango mzuri wa kuudhibiti ugonjwa wa kisukari ni kuufuatilia kwa
makini. Hii ina maana kuwa ni muhimu kufanya kipimo kila siku,
ikiwezekana hata mara mbili au tatu kwa siku. Kutokana na hali hii
gharama za kuufuatilia ugonjwa huu ni kubwa na huathiri kwa kiasi
kikubwa hali ya kiuchumi ya mgonjwa.
Kwa mfano tu, hivi sasa katika zahanati na vituo vingi vya afya, gharama
za kupima kisukari kwa mara moja ni kati ya Sh2,000 na Sh2,500.00.
Unapomwambia mtu apime mara tatu kwa siku maana yake atumie kati ya
Sh6,000 na Sh7,500.00 kila siku.
Ugonjwa wa kisukari kwa sasa kinaonekana kunyemelea hadhi ya kuwa ni
janga la kijamii. Katika pande zote za dunia kisukari kinaongezeka
badala ya kupungua. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), dunia
inatarajiwa kuwa na wagonjwa wa kisukari milioni 366 mwaka 2030 kutoka
wagonjwa milioni 171 waliokuwepo mwaka 2000.
Mwaka 2000 Tanzania ilikuwa na wagonjwa 201,600 na mwaka 2030
inatarajiwa kuongezeka maradufu na kufikia 605,000. Hili ni sawa na
ongezeko la asilimia 66.7.
Hata hivyo janga la kisukari linaoonekana kuzikumba zaidi zile nchi
ambazo raia wao wanapendelea mno vyakula vya wanga katika mitindo
tofauti.
Vyakula hivyo ni soda, pasta, doughnut, keki, mikate, lambalamba,
nakadhalika. Nchi kama Italy uwiano kati ya Wataliano wanaoumwa kisukari
na wale ambao hawaumwi ni mtu mmoja kati ya 14. Inawezekana sababu
kubwa ikawa ni ulaji wa piza, pasta na spaghetti. Hivi ni vyakula
vinavyotengenezwa kwa ngano na Wataliano wanapenda kuvila kwa wingi.
Marekani uwiano wao ni mtu mmoja kwa kila watu 17. Hii nayo ni jamii
ambayo inatumia soda, doughnut, chips, pizza, na vyakula vingine vya
wanga vilivyochakatwa kwa kiwango cha juu. India uwiano wao ni mtu mmoja
kati ya 39. Hawa nao ni mabingwa wa vitu vitamu. Wahindi wanapenda
tamutamu za kila aina na sifa kuu ya vitu hivyo ni wingi wa sukari,
ngano, mafuta na rangi.
Tanzania ina uwiano wa mtu mmoja kati ya 238. Huu ni uwiano mzuri sana
ukilinganisha na nchi tulizotangulia kuzitaja. Sababu ya uwiano huu
mzuri ni nini? Kimsingi sehemu kubwa ya Watanzania ni wala wanga zaidi
kutokana na hali zao za kiuchumi?
Nadhani sababu kubwa ni ukweli kwamba Watanzania wengi ni wakaazi wa
vijijini na kimsingi pamoja na kwamba sehemu kuwa ya chakula chao ni
wanga, lakini kutokana na sababu za kiuchumi, wanalazimika kuula wanga
huo katika mfumo ambao haujachakatwa.