25 May, 2015

WAKATI MWINGINE KAZI ZA HAPA NA PALE ZINAKUNYIMA HATA KUPATA HABARI KWA UHURU, VIVYO NI MUDA WAKO KUPITIA KILICHOANDIKWA KATIKA BAADHI YA MAGAZETI YA HAPA KWETU

ZEEE
MWANANCHI
 Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema matamanio ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ya kuwaletea Watanzania mabadiliko waliyoyakosa ndani ya CCM yanaenda kutimia katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba
.
Mbowe aliyasema hayo jana katika mkutano wa chama wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe jijini Dar es Salaam ambako pamoja na mambo mengine alizindua kitabu cha mambo aliyoyafanya mbunge wa jimbo hilo, Halima Mdee na wimbo maalumu wa msanii wa nyimbo za Injili, Flora Mbasha.
Akizungumza katika mkutano huo uliorushwa moja kwa moja na ITV, Mbowe alisema katika maeneo yote ya nchi, watu wamekata tamaa ya maisha kutokana na uongozi mbaya wa chama tawala, hivyo wako tayari kufanya mabadiliko ya mfumo wa utawala.
“Katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu matamanio ya Mwalimu Nyerere yanaenda kutimia. Watanzania wanataka mabadiliko ambayo wameyakosa ndani ya CCM. Nimezunguka nchi nzima na kubaini kuwa wananchi wanazo sababu na uwezo wa kuyaleta mabadiliko kutokana na kiu waliyonayo,” alisema.
Alitumia fursa hiyo kuzungumzia mchakato wa uandikishaji wapigakura kuwa unahitaji kutazamwa kwa namna nyingine ili kuwatendea haki wananchi ambao wana shauku ya kutimiza haki hiyon ya kikatiba.
“Juzi nilikuwa Mbeya, nimeshuhudia wananchi wakilala katika vituo vya kuandikishia kutokana na hofu waliyonayo kukosa uchaguzi mkuu. Namkumbusha Jaji Lubuva (Damian, mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi) aongeze muda na isiwe siku saba kama ilivyopangwa awali. Kutofanya hivyo atakuwa anajitafutia lawama ambazo hakutakuwa na kiongozi yeyote wa CCM atakayesimama kumtetea pindi wananchi watakapokuwa wanamlaumu hapo baadaye,” alisema.
Mwenyekiti huyo mwenza wa umoja wa Katiba ya wananchi (Ukawa), pia alibainisha mkakati wa umoja huo kugomea na kuipinga rasimu inayotaka vyombo vyote vya habari kujiunga na Shirika la Habari Tanzania (TBC) kwa taarifa ya habari ya saa 2.00 usiku.
“Tutaleta vurugu. Tutasimamisha Bunge kupinga sheria hiyo kwa sababu hiyo ni hujuma ambayo wananchi hawaikubali na mimi kama kiongozi wa upinzani nitalisimamia hilo,” alieleza.
MWANANCHI
Mbio za kuwania urais na nafasi nyingine kupitia CCM zimetangazwa rasmi baada ya Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kutoa ratiba ikibainisha kuwa mgombea urais chama hicho tawala atajulikana Julai 12, siku mbili baada ya yule wa Zanzibar kufahamika.
“Sasa ni ‘ruksa’ kwa wanaotafuta uteuzi wa kupeperusha bendera ya chama katika nafasi za urais, ubunge, udiwani na uwakilishi kuchukua fomu kwa tarehe zilizopangwa,” Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema jana mjini hapa.
Wanaotaka kuwania urais wataanza kuchukua fomu kuanzia Juni 3 hadi Julai 2.
Nape alisema Mkutano Mkuu wa Taifa wa CCM ambao ndiyo wenye jukumu la kuchagua mgombea urais wa chama hicho, utafanyika kwa siku mbili kuanzia Julai 11 hadi 12. Alisema mgombea urais wa Zanzibar, atapitishwa na NEC Julai 10.
Mara baada ya kupitishwa kwa ratiba ya mchakato huo, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho (Bara), Mwigulu Nchemba alijizulu wadhifa huo ili kupata fursa ya kuwania urais.
Naibu Waziri huyo wa Fedha, alimwandikia mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete kuomba kuachia ngazi, naye akampa nafasi kueleza nia hiyo mbele ya kikao.
Akizungumza mkutanoni hapo, Mwigulu alisema amefikia uamuzi huo kwa kuwa hawezi kuwa refa na mchezaji.
Kutokana na uamuzi huo, Rais Kikwete alimteua aliyekuwa msaidizi wake kisiasa, Rajab Luhavi kuwa mjumbe wa Halmashauri Kuu na kuchukua nafasi ya Mwigulu.
Akizungumzia utaratibu wa uchukuaji fomu alisema kwa wanaowania kuteuliwa kugombea urais wataanza kuchukua fomu hizo Juni 3, mwaka huu na mwisho wa kuzirejesha ni saa 10.00 jioni ya Julai 2.
Alisema muda huo wa Juni 3 hadi Julai 2, pia utatumika kwa wagombea urais kutafuta wadhamini 450 katika mikoa 15, kati ya hiyo mitatu ikiwa ya Zanzibar, kwa maana ya Pemba na Unguja.
Utaratibu wa zamani kwa wagombea uliwataka kuwa na wadhamini 250 katika mikoa 10, miwili iwe ya Zanzibar. Pemba mmoja na mwingine Unguja.
Alisema hatua hiyo ya wadhamini 450 imetokana na kuongezeka kwa idadi ya wanachama na mikoa na kwamba idadi hiyo haitakiwi kupungua wala kuzidi.
MWANANCHI
 Ni dhahiri sasa michezo ya kubahatisha hapa nchini imeshika kasi kutokana na ongezeko la vituo vya kamari ya soka maarufu kama ‘kubeti’.
Kamari hizi zilizowateka watu wa jinsi na rika zote, kwa sasa zimeshika kasi huku vituo vya kuchezesha vikichipuka kama uyoga katika maeneo mengi ya Dar es Salaam.
Vituo maarufu ni Premier Betting na Meridian Betting, ambavyo vyote vipo katika ushindani mkubwa wa kuchezesha mchezo na kuvuta watu wengine jijini.
Mkurugenzi wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania, Abbas Tarimba alisema michezo hiyo imekuwa chanzo kikubwa cha mapato kwenye bodi hiyo na kuongeza mzunguko wa fedha unaozidi Sh2 bilioni kwa mwezi.
Alisema michezo hiyo ya kubahatisha inafanya vizuri, kwani mapato yake kwa bodi hiyo hufikia Sh1.4 bilioni kwa mwaka.
Alisema wamiliki wa vituo vya kamari hizo ni lazima wafuate kanuni zilizoainishiwa na bodi ya michezo ya kubahatisha nchini.
Tarimba alisema matatizo kadhaa yanayojitokeza kwenye michezo hiyo ni pamoja na malalamiko ya kutotendewa haki kwa wachezaji.
Mfanyabiashara wa genge, eneo la Tabata, Mawenzi, Yohana Ibrahim alisema ameanza kucheza kamari hiyo mwaka huu na ameshashinda mara nyingi.
“Nimeshawahi kushinda Sh200,000 mara mbili, nimeshinda 70,000, 50,000 na hizi Sh10,000 ndiyo mara nyingi,” .
Ibrahimu ambaye mara nyingi ‘hubeti’ kwenye kampuni ya Meridian, alisema ingawa anakosa mara moja moja, lakini mara nyingine amekuwa akishinda na kujipatia fedha ambazo huziingiza kwenye biashara yake ya genge.
MWANANCHI
Mamlaka ya udhibiti wa chakula na dawa Tanzania TFDA imefunga machinjio 11 ya kuku na ng’ombe jijini Dar es salaam kutokana na kudaiwa kukithiri kwa uchafu na kuwa na miundombinu mibovu.
Machinjio hayo yalifungwa tangu Mei 13 baada ya Mamlaka hiyo kukagua na kufanya ukaguzi na kugundua  mazingira machafu, jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa afya za walaji.
Afisa uhusiano wa Mamlaka hiyo Gaudensia Simwanza alisema jana kuwa wamelazimika kufunga machinjia hizo baada ya kutoridhishwa na hali ya usafi waliyoikuta.
Kule ndiko wanyama wanachinjwa, nyama zinanunuliwa  na kupelekwa buchani, lakini mazingira ya eneo lote ni machafu, walaji hawawezi kuwa salama.
Alisema katika baadhi ya machinjio wahusika wameonyesha jitihada za kufanya usafi na kuboresha miundombinu yao ikiwa ni pamoja na kuzibua mifereji ya kupitisha maji machafu.
Uamuazi huo wa TFDA umelalamikia na wafanyabiashara hiyo wakidai wamewatia hasara. Karibu siku ya 10 sasa hatuna sehemu ya kwenda kuchinjia ng’ombe, hivi wanafikiri tutaishi vipi wakati tuna familia zinazotutegemea? walihoji
HABARILEO
Kauli nzito na thabiti ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake ya ufunguzi wa Kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama hicho, juzi imewagusa wengi na kusifu huku wakisema imejaa busara, hekima na ukomavu wa hali ya juu wa kioungozi.
Katika hotuba yake, Kikwete alikitaka chama kusimama imara na kuhakikisha kinapitisha wagombea wanaokubalika na wananchi wote huku akisisitiza kuwa, chama chake kamwe hakitachagua mgombea kwa shinikizo la mtu yeyote, bali kitasimamia misingi bila ya woga, huku akisisitiza kuwa;
“Tupeleke kwa wananchi wagombea ambao hawana shaka nao…lazima tusome alama za nyakati, mgombea wetu awe ni yule anayeakisi mambo yanayochukiza watu.
“Wakati wa Wana-CCM kujidanganya kuwa tunapendana umepitwa na wakati kwani wananchi hawatasita kuona wanayependezwa naopenwngombea,” alisema na kuweka bayana kuwa, kuna wagombea wanaokosea misingi ya chama, hivyo kuwataka kuelewa kuwa, chama ndicho kinachosimama mbele badala ya mtu.
Kauli za Mwenyekiti huyo wa CCM zimekuja huku baadhi ya makada wa chama hicho wakipigana vikumbo ndani na nje ya chama ili kujenga ushawishi wa kuonekana wanakubalika na hatimaye waweze kupitishwa na chama hicho tawala kuwania Urais na nafasi nyingine za uongozi wa dola katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Habari kutoka ndani ya chama hicho zinasema baadhi ya wenye nia ya kuwania Urais, licha ya kuingia Dodoma kwa mbwembwe wakiwa na wapambe wenye utajiri mkubwa wa fedha, walinywea huku wapambe wao wakiondoka mjini humo kimyakimya.
Lakini kwa kiasi kikubwa, baadhi ya wanaotajwa kutaka kuwania urais, nao walielezea kufurahishwa, wakisema imeangalia zaidi maslahi ya chama na nchi kwa ujumla.
Watangaza nia Urais Akizungumza na gazeti hili, mbunge wa Sengerema William Ngeleja ambaye tayari ametangaza nia ya kugombea, alisema kauli hiyo ya Rais Kikwete imetoa mwelekeo na kusisitiza umuhimu wa taratibu, kanuni na Katiba ya chama kuzingatiwa.
Naye Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, alisema kwa kauli hiyo ya Rais Kikwete, ni dhahiri kuwa ipo dhamira ya dhati ya viongozi wa CCM ya kusaidia chama hicho kumpata mgombea msafi ambaye hatakuwa na haja ya kumtetea au kumtolea maelezo ya kumnadi.
Nimefurahishwa sana na nampongeza Rais kwa kauli yake, nimefurahi kwamba mwenyekiti anaamini kuwa hatuwezi kuteua mgombea wetu kwa kujisahaulisha yaliyotokea nyuma,” January.
NIPASHE
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Wilbroad Slaa amewataka waandikishaji na wasimamizi wa uandikishaji wa wananchi kielektroniki katika daftari la kudumu la wapiga kura (BVR), kutoa kipaumbele kwa kina mama wajawazito, wazee, wagonjwa na walemavu, ili waweze kujiandikisha bila kupata madhara.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kata ya Hamugembe jana baada ya kuzunguka kwenye baadhi ya vituo vya uandikishaji, Dk. Slaa alisema kuwa kitendo alichokutana nacho katika manispaa ya Bukoba cha kukuta mama mjamzito amezimia kutokana na kukaa kwa muda mrefu katika mstari bila kuandikishwa, hajafurahishwa nacho.
Kama waandikishaji na wasimamizi wa zoezi hili hawafahamu vizuri sheria ya uchaguzi, basi waitafute waisome ili waelewe kuwa makundi haya ya watu hayapaswi kukaa katika mistari muda mrefu, badala yake inabidi wanapofika wahudumiwe na kuondoka,” alisema.
Kutokana na hali hiyo alimwagiza mwenyekiti wa Chadema Bukoba mjini, Victor Sherejey, kufuatilia katika vituo vyote na kuhakikisha kasoro zilizobainika zinafanyiwa kazi, ikiwamo ya makundi hayo ya watu kuandikishwa bila kusumbuliwa.
Alisema kuwa kila mwananchi mwenye sifa bila kujali hali aliyonayo anapaswa kuandikishwa na kuwa hiki ni kipindi kigumu kuliko vipindi vyote maana uandikishaji ndiyo mwanzo wa kupiga kura, ambaye hatajiandikisha hawezi kulalamika baadaye dhidi ya viongozi wasiofaa watakaochaguliwa.
Aidha Dk. Slaa alizungumzia sheria inayolenga kukandamiza uhuru wa vyombo vya habari na kuwa kitendo cha serikali kuandaa kupeleka bungeni muswada wa sheria ya habari kwa hati ya dharura, kuzifunga redio na vyombo vingine, zisitangaze matokeo ya uchaguzi, ili serikali  iliyoko madarakani iweze kufanikisha azma yake ya kuiba kura.
“Serikali ina maana gani kuzitaka redio binafsi zijiunge na redio ya taifa kila ifikapo saa mbili, muda huo watu ndipo wanakuwa wametoka kuhangaika na shughuli za hapa na pale wanataka kutulia kusikiliza taarifa za ukweli kutoka vyombo mbalimbali, leo hii serikali inasema redio zote zijiunge na redio ya taifa, huu ni ukandamizaji wa vyombo vya habari,”.
Aliitaka serikali kutowafunga midomo waandishi wa habari hasa katika kipindi hiki cha uchaguzi mkuu, maana wananchi wa Tanzania wana haki ya kupata habari sahihi na kwa wakati wanaotaka.
NIPASHE
Mkuu wa Chuo Kikuu Huria Tanzania (OUT), Dk. Asha-Rose Migiro, ameshushiwa tuhuma nzito za kurudisha nyuma maendeleo ya chuo hicho kutokana na hatua yake ya kutomtangaza makamu mkuu mpya wa chuo hicho kuziba nafasi iliyoachwa na Prof. Tolly Mbwette aliyestaafu mwezi uliopita.
Hivi sasa, nafasi ya makamu wa chuo hicho inakaimiwa na Prof. Elifas Bisanda. Hata hivyo, ilielezwa na baadhi ya watumishi kuwa kuna hofu kubwa ya kurudi nyuma kitaaluma kwani baadhi ya mambo hayafanyiki vizuri kutokana na kukosekana kwa mrithi rasmi wa Mbwette.
Aidha, ilielezwa zaidi kuwa mchakato wa kumpata makamu mpya wa chuo hicho ulishaanza Aprili, 2014 na mapendekezo yalishafikishwa kwa Dk. Migiro, lakini mkuu huyo ambaye pia ni Waziri wa Sheria na Katiba bado anasita kumtangaza mrithi wa Mbwette kwa sababu anazozijua yeye.
Kwa mujibu wa Sheria ya Vyuo Vikuu ya mwaka 2015, Mkuu wa Chuo ndiye mwenye mamlaka ya kuteua Makamu Mkuu wa Chuo.
Kwakweli hofu imetanda. Mambo yameanza kwenda kombo… kuna maamuzi makubwa yenye manufaa kwa chuo yanashindwa kufanyika kwa sababu ya kukosekana kwa makamu mkuu wa chuo,” alisema mmoja wa wafanyakazi wa chuo hicho chenye matawi nchini kote na pia kikiwa pekee chenye matawi katika nchi za Kenya, Uganda, Rwanda, Namibia na Malawi.
Inadaiwa kuwa hivi sasa, tayari baadhi ya wahadhiri wanafikiria kuhamia vyuo vingine kwa sababu mambo mengi yamesimama katika kipindi hiki cha kukosekana kwa makamu mkuu wa chuo.
“Kinachotushangaza ni huu ukimya unaoashiria picha mbaya kuwa labda chuo kinakosa watu wenye sifa. Kila mmoja anajua kuwa vetting (mchakato wa kuwapata wateule) ilishafanyika kwa mwaka mzima na majina alishapewa… sasa sijui (Dk. Migiro) anakwama wapi,” kilieleza chanzo kimoja kutoka chuoni hapo.
Taarifa zaidi zilidai kuwa Dk. Migiro ana mtu wake ambaye siyo miongoni mwa majina aliyopewa na ndiyo maana anasita kutumia mamlaka yake ya kumtangaza makamu mkuu wa OUT, kama anavyopaswa kufanya kwa mujibu wa Sheria ya Vyuo Vikuu ya mwaka 2005.
Baadhi ya wafanyakazi wa OUT walieleza kuwa miongoni mwa athari za kutokuwapo kwa makamu mkuu rasmi wa chuo chao ni pamoja na kutoagwa kwa mkuu aliyemaliza muda wake (Prof. Mbwette) kwani kwa kawaida jambo hilo hufanyika baada ya kutangazwa kwa makamu mpya.
“Na athari kubwa zaidi ni matumizi mabaya ya rasilimali za chuo. Hivi sasa kuna wakubwa husafiri kila mara na hakuna wa kuwazuia kwa sababu aliye madarakani (kaimu makamu mkuu) hawezi kufanya maamuzi magumu… na hili liko wazi tu kwa sababu yeye (kaimu makamu) hana uhakika wa kuendelea kubaki katika nafasi hiyo. Hajui pengine huyo atakayemuadhibu leo ndiye kesho anakuwa bosi wake,” chanzo kingine kiliongeza.
Akizungumzia hali hiyo ya kukosekana kwa makamu mkuu wa OUT, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Anne Kilango Malecela, alisema suala hilo halipo tena wizarani kwao na hivyo aulizwe mkuu wa chuo hicho, Dk. Migiro.
NIPASHE
Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima, jana aliibukia kwenye mkutano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Jimbo la Kawe, Dar es Salaam.
Mkutano huo ulikuwa wa uzinduzi wa kitabu cha kazi alizofanya Mbunge wa jimbo hilo na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), Halima Mdee.
Askofu Gwajima alionekana kwenye jukwaa kuu na viongozi mbalimbali wa Chadema, akiwamo mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, katika mkutano uliofanyika katika viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe, jijini Dar es Salaam.
Miongoni mwa watu wengine  maarufu waliokuwapo kwenye mkutano huo ni mwimbaji wa nyimbo za injili, Flora Mbasha, ambaye aliimba wimbo maalum kwa ajili ya chama hicho na ulizinduliwa jana.
Mkutano huo ulitanguliwa na maonyesho ya kikundi cha ulinzi cha Chadema  (Red Brigade) na baadaye wimbo maalum wa amani na pongezi kwa chama hicho ulioimbwa na Mbasha na kuamsha shamrashamra kwa watu waliohudhuria ikiwamo kupanda jukwaani kucheza.
Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Mbowe, akihutubia mamia ya wananchi wa jimbo hilo, alisema uchaguzi wa mwaka huu ndiyo matamanio ya baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, ambayo alikuwa nayo wakati wa siku za mwisho za uhai wake.
Mwalimu Nyerere alisema: “Watanzania wanataka mabadiliko, wasipoyapata ndani ya CCM watayatafuta nje ya CCM,” sasa wakati wa kuyatafuta nje ya CCM  umefika na Watanzania kwa kushirikiana na Ukawa na wananchi wasio na chama lakini wana mapenzi mema na nchi wanaungana nasi.”
Mbowe alisema baada ya kutembea nchi nzima amegundua Watanzania wanayataka mabadiliko, wana uwezo wa kuyaleta na wako tayari kuyaleta, utayari ambao hauipi amani CCM na kudai ndiyo maana ina haribu mfumo wa uandikishaji wapigakura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa mfumo wa Biometric Voters Registration,” alisema.
Alisema juzi alitembelea vituo vya uandikishaji mkoani Mbeya katika wilaya ya Rugwe Tukuyu, Kyela na alibaini Watanzania wanalala kwenye vituo vya kujiandikisha kwa sasabu vifaa havitoshi na imefanyika hivyo makusudi ili Watanzania wengi wasiandikishwe.
Naomba kupitia mkutano huu nimshauri Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Jaji Damian Lubuva, lawama utakayoipata kutokana na BVR, CCM hawatakuwa na wewe, wanakutumia kwa sasa, kikiwaka utawekwa kando,” alitahadharisha na kuongeza:
Vifaa (BVR Kits) havitoshi, tunakuomba (Jaji Lubuva) utangaze umeongeza siku za kujiandikisha na siyo siku saba ili wenye sifa wajiandikishe.
“Nimeshuhudia kinamama wanalala vituoni kwa sababu uandikishaji umekuwa adhabu kwao,” alidai.
Mwenyekiti huyo wa Chadema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Ukawa, alisema wapigakura wengi wanaunga mkono mabadiliko na wakijiandikisha itakuwa ni kaburi kwa CCM na kuongeza:
Mbowe alisema uchaguzi mkuu kikatiba unatakiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu na kwamba kwa sasa zimebaki siku 121 kufika siku hiyo na Nec haijatangaza majimbo ya uchaguzi na uwakilishi pamoja na ratiba ya uchaguzi.
Kwa mujibu wa Mbowe, serikali itakayoundwa na Ukawa itaongoza taifa katika misingi ya kurudisha utawala wa haki na sheria ili kurudisha matumaini kwa wananchi wote.
Aidha, aliwataka watumishi wa umma kutokuwa na hofu kwani Ukawa haingii kubadili au kufukuza mtu kazi, bali kufanya mabadiliko makubwa kwa Watanzania na kwamba kitakachobadilika ni vyama vinavyoongoza nchi na siyo mifumo ya utawala.
Akizungumza na hadhara hiyo baada ya Mbowe kumaliza kuhutubia, Askofu Gwajima alisema hotuba ya Mbowe ina ujumbe mzito na kwamba ana amini aliyozungumza kaongozwa na Mwenyezi Mungu kuyazungumza kwa ajili ya umma.
Alisema anatambua kuwa Chadema ina thamini mabadiliko na kutoa baraka kwa chama hicho kuendelea na jitihada hizo kwa kuwa wakati wa ukombozi umewadia.

NI HAPA HAPA MTOKA MBALI, ENDELEA KUTUFUATILIA KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK: Mawere Mtoka Mbali, TWITTER:@mawere3,INSTAGRAM: MAWERE_MTOKI_MBALI, SUCRIBE YOUTUBE:MAWERE TV. AKSANTE NA ENDELEA KUTEMBELEA MTOKA MBALI

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...