15 May, 2015

Ndesamburo ilivyotumia Sh1b kutoa ajira kwa vijana 1,000

 Image result for Ndesamburo
Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo, anaweza kuingia katika vitabu vya kumbukumbu kutokana na staili yake ya kuuaga uwanja wa kisiasa kwa kutazama tatizo la ajira kwa vijana, ambalo ni tatizo sugu na limekuwa likizungumziwa kisiasa kama bomu linalosubiri kulipuka.Alipowaaga wananchi wake kwa kuwaachia kitega uchumi chenye thamani ya zaidi ya Sh1 bilioni.
Ndesamburo, amekuwa mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini kwa vipindi vitatu mfululizo; yaani kuanzia mwaka 2000 hadi 2015 na sasa ametangaza rasmi kutogombea ubunge.
Hoja hapa siyo kustaafu ubunge, ila ni staili aliyoitumia kustaafu pale alipoamua kujenga soko la kisasa na kuliita “Kiborlon Shopping Centre” na kuwapa hisa wafanyabiashara kadhaa wadogo, maarufu kama Wamachinga.
Ndesamburo anasema amejenga soko hilo kubwa kuliko yote katika mikoa ya Kaskazini, kama njia ya kutatua tatizo la muda mrefu la wafanyabiashara wadogo na kati. Soko hilo lina runinga kubwa katika mlango wake mkubwa ikiwa na stesheni mbalimbali za televisheni na lina vibanda zaidi ya 200 vya maduka na eneo la kuchukua “Machinga” na wauza mitumba 1,000.
Ujenzi wakwepa fitina za kisiasa
Ndesamburo anasema isingekuwa rahisi kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati kujikusanya na kuchanga fedha za kujenga soko hilo la kisasa.
“Tatizo la maeneo ya kufanyia biashara kwa Machinga na wafanyabiashara wa kati ni kubwa sana na nilipokuwa mbunge kwa mara ya kwanza mwaka 2000 niliahidi kushughulikia tatizo hili,” anasema.
Anasema alibaini Halmashauri ya Manispaa ya Moshi wakati huo ikiongozwa na CCM, ilikuwa haina mpango wa kutenga eneo kwa ajili ya Wamachinga na kwamba hata mikakati iliyowekwa ilikuwa ni ya muda na haiwasaidii wengi.
“Hapo ndipo niliponunua eneo hili na kutoa wazo kwa Serikali kwamba kwa kupitia mpango wa PPP (ubia serikali na sekta binafsi) tujenge soko la kisasa la Mitumba na Machinga,” anasema Ndesamburo.
Ndesamburo anasema wazo lake hilo lilikataliwa na viongozi wa Serikali ya CCM kwa sababu za kisiasa kwamba kama kungejengwa soko la wafanyabiashara hao, basi jina lake lingepanda chati.
“Kwa sababu ya vita kubwa ya kisiasa ndani ya Jimbo letu nikaamua nijenge mwenyewe lakini swali likawa je, hawa madiwani wa CCM wangekubali kunipitishia michoro ya soko?” Anasema akifafanua:
“Nikachora ramani na ikapitishwa kwa jina la mhindi. Sikutumia jina langu kwa sababu kama ningelitumia wasingekubali,” anasema Ndesamburo ambaye pia ni mfadhili wa Chadema.
“Nilipoanza kutaka kujenga, usalama wa Taifa, Gama na Manispaa wote walikuja hapa kuzuia nisijenge lakini wakati huo tayari nilishakuwa na vibali vyote vya ujenzi kwa jina la Mhindi.”
‘Vita vya panzi’
Ndesamburo alidai pamoja na soko kukamilika, lakini wapo makada wa CCM ambao wameshika vyumba vya biashara lakini hawavifungui ili dhana ya kuwapo kwa soko isiwepo.
“Nimesema yeyote asiyefungua tutawapa watu wengine. Yeyote ambaye hata kama amelipa deposit (dhamana) tunamnyang’anya na tutakata fedha yetu ya kukodisha,” anasema Ndesamburo.
Mbunge huyo anasema ametoa ‘ofa’ kutoka sasa hadi Julai Mosi, mwaka huu, wafanyabiashara waliochukua maeneo ya biashara katika soko hilo wafanye biashara bure na baada ya hapo ndiyo wataanza kulipa kodi.
Ndesamburo anasema wafanyabiashara wote watakaomuunga mkono kwa kufungua biashara zao kuanzia jana, watakuwa wana hisa wa soko hilo ili kuondoa propaganda chafu alizodai zinaenezwa na CCM. “CCM wanapita huko na huko wanasema hiki ni kitega uchumi cha mtu binafsi lakini mimi nasema hawa waliokodi vibanda hapa watakuwa wanahisa. Tutaendesha pamoja hili soko,” anasema.
“Siyo hivyo, lakini nimeamua kuagiza mitumba moja kwa moja kutoka Ulaya kwa wafanyabiashara watakaotumia soko hili. Bei yake itakuwa chini ya wanaonunua hapa nchini.”
Kodi ni mzozo
Pamoja na ofa nyingi zilizotolewa na Ndesamburo baadhi ya wafanyabiashara, wanaona kodi ya Sh100,000 kwa mwezi kwa vibanda katika soko hilo ni kubwa na kutaka ipungue hadi Sh50,000 kwa mwezi. Hamisi Shemdoe ni mfanyabiashara wa kutembeza viatu na anasema anatamani kukodisha kibanda, lakini hawezi kumudu kodi ya Sh100,000 kwa mwezi labda angepewa kwa Sh30,000 au 50,000.
Hata hivyo, Ndesamburo mwenyewe anasema milango ya majadiliano haijafungwa, hivyo wale wenye maoni na michango ya namna ya kuboresha huduma za soko hilo, wako huru kumuona.
Pamoja na mipango hiyo, watu wengi wana wasiwasi kwamba chokochoko za kisiasa zinaweza zikakwamisha uzuri na shughuli za kibiashara katika soko hilo.Hayo yanazungumzwa huku kukiwa na imani kwamba kwa kuwa soko hilo limejikita kwa faida ya jamii, siasa kamwe hazina nafasi.


Mawerenewz.blogspot.com ndio mtandao wako wakipekee unaokupa habari za BURUDANI,MICHEZO, SIASA, na HABARI MBALIMBALI ZA KIMATAIFA pamoja na KITAIFA Endelea kutembelea MTOKA MBALI pia nifuate twitter>>>@mawere3, facebook>>>Mawere Mtoka Mbali, Instagram>>>mawere_mtoka_mbali,SuScribe Youtube>>>MAWERE TV

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...