11 May, 2015

MAGAZETINI LEO MAY 11

Image result for NEWS UPDATENIPASHE
Hali ndani ya Chama cha Tanzania Labour Party ‘TLP’ imezidi kuwa tete baada ya Mwenyekiti wake Augustino Mrema kuwafuta wanachama wake 10 kwa madai kuwa wanakisaliti chama.
Hata hivyo wanachama waliofukuzwa hawakuweza kupatikana kuelezea ni sababu gani zilizosababisha wafukuzwe na
ni taratibu zipi watachukua dhidi ya Mrema kutokana na uamuzi wake wa kuwafukuza.
Mrema alisema wanachama hao walifukuzwa uanachama kufuatia kikao cha Sekretarieti ya Chama iliyokutana Mei 7 kujadili mambo mbalimbali ikiwemo uasi unaofanywa na baadhi ya wanachama ndani ya chama hicho.
Alisema watu hao waliunda kikundi hicho kinachojiita cha Ukweli na Maridhiano ambacho kimekuwa kikiendesha harakati za kuendesha uasi na kuonyesha kuwa kuna mpasuko ndani ya chama wakati haupo.
MTANZANIA
Chama cha Wananchi (CUF), kimetoa matokeo ya utafiti wake kuhusu Daftari la Wapiga Kura Zanzibar ikieleza kuwa watoto wasiotimiza umri wa miaka 18 na watu waliofariki dunia, majina yao yanaendelea kutumika katika dafrati hilo huku Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ikikaa kimya.
Kutokana na hali hiyo CUF kimesema kinashangazwa na hatua ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kuandaa mipango kinayodai ni ya kuendelea kuhujumu upigaji kura kwa kutumia vyombo vya ulinzi ambavyo hutoa watu kutoka Tanzania Bara.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, alidai CCM imekuwa ikiandaa njama za hila kwa msaada wa ZEC kuandikisha vijana wasiokuwa Wazanzibari kinyume cha sheria.
Alisema pamoja na hali hiyo, bado kuna haja kwa Wazanzibari kuendelea kushikamana kuhakikisha wanaunga mkono wimbi la mabadiliko Visiwani humo.
“Hivi sasa CCM inatumia kambi za Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) iliyopo Chukwani kuandikisha vijana wasiokuwa Wazanzibari na kuwapatia vitambulisho vya Mzanzibari mkaazi (ZAN IDs) kwa ajili ya kujiandikisha kama wapiga kura.
CUF kimemtaka Rais Dk. Ali Mohamed Shein ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kujiandaa kisaikolojia kukabidhi nchi kwa Makamu wake wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad.
Akijibu swali katika mkutano huo, Maalim Seif alikiri kwa mara ya kwanza kushindwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
“Tukumbuke kwamba kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa mwaka 2010 yalifanyika kwanza maridhiano hali iliyosababisha kufanyika uchaguzi huru, haki na wa amani na hakuna hata nzi aliyebanwa katika kipindi cha kampeni.
Kuhusu suala la yeye kugombea urais katika kila uchaguzi, Maalim Seif alisema CUF kimekuwa kikitoa fursa kwa kila mwenye sifa kuchukua fomu lakini hawajitokezi.
MTANZANIA
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, amesema ni muhimu kwa Tanzania kukimbia kwa kasi ili kukabiliana na changamoto za maendeleo ya kisanyansi duniani.
Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli (CCM), aliyasema hayo jana alipokuwa akihutubia katika sherehe za Jubilee ya miaka 25 ya uaskofu na miaka 40 ya upadri ya Askofu Paul Ruzoka wa Jimbo Kuu Katoliki la Tabora.
Kwa mujibu wa Lowassa, elimu ya Tanzania inakabiliwa na changamoto nyingi na kwamba njia sahihi ya kukabiliana na changamoto hizo ni kwenda na kasi ya maendeleo duniani.
“Ni wazi kwamba, mabadiliko haya makubwa yametufikisha mahali ambako sisi kama taifa tunapaswa kuchukua hatua za kuruka ili kuweza kukabiliana na kasi kubwa ya maendeleo yanayotokea duniani hivi sasa.
“Maendeleo hayo makubwa yanapaswa yawe darasa la kuirejesha Tanzania katika falsafa ya elimu ya kujitegemea kwani elimu hiyo inajenga misingi imara kwa wahitimu wanaomaliza shule na vyuo kuanzia kidato cha nne na kuendelea ili waweze kujiajiri au kuajiriwa katika sekta mbalimbali,” Lowassa.
Pamoja na hayo, Lowassa ambaye amekuwa mdau wa elimu nchini, alilipongeza Kanisa Katoliki kwa mchango mkubwa linaoutoa katika maendeleo ya elimu nchini.
MTANZANIA
Chama cha Mapinduzi (CCM) kimetangaza ratiba ya vikao vya chama hicho kuanza mwezi huu ikionyesha mchakato wa kuchukua fomu za kuwania kugombea urais utafanyika wakati makada wake sita waliofungiwa wakiendelea kuwa kifungoni.
Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema baada ya ratiba ya uchaguzi kutangazwa ndani ya chama hicho, wana CCM watatakiwa kuendelea kuheshimu taratibu na sheria za chama chao.
Februari 18, mwaka jana CCM iliwapa adhabu ya kifungo cha mwaka mmoja makada wake sita wa chama hicho ambao walidaiwa kuanza kampeni mapema za urais nao ni Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushiriano wa Kimataifa Bernard Membe, Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye, Mbunge wa Sengerema William Ngeleja, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira pamoja na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia January Makamba.
“Umeuliza kama ratiba ikitoka wanakuwa huru, nasema hapana. Kama wasipofunguliwa maana yake wanaendelea kubaki kifungoni, wakibaki kifungoni maana yake hawaruhusiwi kushirki mchakato, mfungwa hapigi kura, hiyo ndiyo CCM ni zaidi ya ujuavyo.
Jana, Nape alikaririwa na vyombo vya habari akisema CCM itaanza vikao vyake Mei 18 hadi 22 mwaka huu mjini Dodoma.
Alisema vikao hivyo vitajadili ratiba ya mchakato wa uteuzi wa wagombea udiwani, uwakilishi, ubunge, urais wa Zanzibar na urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
MWANANCHI
Kuna kila dalili kwamba Chadema na vyama washirika vina mpango wa kumsimamisha Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kugombea urais Oktoba mwaka huu.
Dalili hizo zilijitokeza hadharani juzi kutokana na kauli ya Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu aliyoitoa katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Viwanja vya Majengo, Moshi akimtaja Dk Slaa kama ndiye rais ajaye huku akieleza uwezekano wa Ukawa kuchukua nchi.
Lissu alimtaja Dk Slaa na Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo kuwa ndiyo wabunge wa Chadema ambao hawajawahi kushindwa na CCM tangu mwaka 1995.
“Historia hiyo itasema mbunge mmoja kati yao  ni Mzee Ndesamburo na historia hiyo itasema mbunge wa pili ambaye hajawahi kushindwa na CCM ni Dk Willibrod Slaa, rais wetu ajaye,Lissu.
Mjumbe huyo wa Kamati Kuu (CC) ya Chadema, alisema katika historia ya Taifa hili kuna uwezekano mkubwa wa Chadema na vyama washirika kuingia Ikulu baada ya Oktoba.
Vyama washirika ambavyo vinaunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD, vimepanga kusimamisha mgombea mmoja katika ngazi zote za uchaguzi kuanzia urais hadi udiwani katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Dk Slaa aligombea urais 2010 na kushika nafasi ya pili kwa kupata kura milioni 2.3 sawa na asilimia 26.34 nyuma ya Rais Jakaya Kikwete aliyeshinda kwa kura milioni 5.3 sawa na asilimia 61.17.
Hadi sasa Ukawa haijateua wagombea wake katika ngazi hizo ambazo ni urais, ubunge na udiwani ambao watachuana na wagombea wa vyama vingine.
Katika hotuba yake hiyo, Lissu alisema: “Katika miaka 20 ya kwanza ya mfumo wa vyama vingi, kuna wabunge wawili pekee ambao hawajawahi kushindwa na CCM.”
HABARILEO
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Kasukulo Sambo juzi alinusurika katika mapambano yaliyoibuka eneo la Soko Kuu mjini hapa mkoani kati ya askari polisi na madereva wa pikipiki za magurudumu matatu maarufu kama Bajaj, baada ya madereva hao kugoma na kufunga barabara kwa kulala kifudifudi.
Kitendo hicho kilisababisha kusimama kwa huduma ya usafiri katika barabara kuu inayounganisha mji ya Sumbawanga na Tunduma kwa saa kadhaa na kusababisha askari polisi kufyatua risasi hewani na kurusha mabovu ya machozi ili kuwatawanya.
Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) walifika eneo hilo la tukio wakiwa na silaha nzito wakitumia usafiri wa gari lao  tayari kukabiliana na mgomo huo .
Licha ya madereva hao kulala kifudifudi barabarani, pia waliweka mbao zilizopigiliwa misumari kuzuia gari lolote lisipitie eneo hilo la tukio na kuchoma matari ya magari.
Miongoni mwa watumiaji wa barabara waliokumbwa na adha hiyo ni Jaji Sambo ambaye gari lake lilizuiwa na kunusurika kushambuliwa na madereva hao waliokuwa wamejawa na ghadhabu.
 Jaji Sambo alithibitisha kutokewa na mkasa huo na kwamba maofisa askari wa usalama barabarani waliingilia kati na hatimaye akaruhusiwa kupita eneo hilo na gari lake .
Nilipofika eneo hilo nilikuwa madereva wa bajaji wakiwa wamegoma wakitaka kuonana na Mkuu wa Mkoa kwa kufunga barabara kuu …..walinizuia nisipite hadi askari polisi wa usalama barabara alipoingilia kati pia mlinzi wangu alilazimika kushuka gari akiwa tayari na bastola kwa kujihami…. “Hatimaye niliweza kupita hapo salama saliminik lakini mkasa huo umesababisha adha kubwa kwa watumiaji wengine wa barabara,“ Jaji Sambo.
Shughuli za kawaida katika soko kuu la mjini Sumbawanga zilisimama kwa muda wa saa moja baada ya jeshi la polisi mjini hapo kuvutana juu ya mgomo wa ghafla ulioitishwa na madereva wa pikipiki za magurudumu matatu maarufu kwa jina la bajaji.
Kaimu Kamanda Polisi mkoa wa Rukwa, Kamishina Msaidizi wa Polisi, Leons Rwegasira amethibitisha kutokea kwa vurugu hizo na kueleza kuwa bado jeshi hilo linatumia busara kulishughulikia tatizo hilo kabla ya kuanza kamata kamata.
HABARILEO
Rais Jakaya Kikwete ameitisha mkutano wa wakuu wenzake wa nchi tano za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ili kujadili hali ya Burundi.
Ameitisha mkutano huo wakati Burundi ikiripotiwa kuwa katika vurugu zinazotishia hali ya usalama, hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa mwezi ujao.
Rais Kikwete amechukua uamuzi huo kwa wadhifa alionao wa Mwenyekiti wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Alitangaza kuitisha mkutano huo wakati alipozungumza na waandishi wa habari katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa (UN), kuwaelezea matokeo ya mkutano wa wiki moja wa Jopo la Watu Mashuhuri Duniani, linaloangalia jinsi dunia inavyoweza kukabiliana na majanga ya kiafya katika siku zijazo kufuatia balaa la ugonjwa wa ebola katika Afrika Magharibi.
Rais Kikwete na wana-Jopo wenzake walizungumza na wanahabari juzi jijini New York, baada ya kuwa wamemaliza kikao cha kwanza cha Jopo lao lililoteuliwa na Katibu Mkuu wa UN, Ban Kimoon, Aprili 2, mwaka huu, 2015, kupendekeza jinsi dunia inavyoweza kukabiliana na majanga ya kiafya, na hasa ya magonjwa ya mlipuko, katika siku zijazo kufuatia balaa na athari za ugonjwa wa ebola katika Afrika Magharibi.
Ugonjwa wa ebola umeua watu karibu 10,000 katika kipindi kifupi katika nchi za Guinea, Liberia na Sierra Leone. Ugonjwa huo ulijitokeza kwa mara ya kwanza mwaka 1976, karibu miaka 40 iliyopita katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Mpaka sasa ugonjwa huo hauna dawa inayojulikana dhahiri wala chanjo.
Katika maswali yaliyofuatia maelezo yake na ya wanajopo wenzake kuhusu kazi yao ya wiki moja, Rais Kikwete aliulizwa kuhusu hali ilivyo katika Burundi na Tanzania, kama jirani inachukua hatua gani kukabiliana na hali hiyo katika nchi jirani.
Rais Kikwete alisema baada ya mawaziri wa nchi za nje wa Tanzania, Kenya, Uganda na Rwanda kuwa wametembelea Burundi majuzi, kwa maelekezo yake, na kumaliza ziara yao kwa kujionea hali ilivyo katika nchi hiyo, ameamua kuitisha Mkutano wa Wakuu wa Nchi za EAC jijini Dar es Salaam, ambako mawaziri hao watatoa ripoti yao ili ijadiliwe.
“Tumekubaliana kuwa sisi ndani ya EAC – Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi yenyewe tukutane Dar es Salaam, Jumatano ijayo, Mei 13 (keshokutwa), ili tujadiliane jinsi gani ya kuwasaidia ndugu zetu wa Burundi kuandaa uchaguzi wao kwa mafanikio, wakihakikisha kuwa nchi yao inabakia na umoja, utulivu, usalama na amani bila misukosuko isiyokuwa na sababu,” Rais Kikwete.

Mawerenewz.blogspot.com ndio mtandao wako wakipekee unaokupa habari za BURUDANI,MICHEZO, SIASA, na HABARI MBALIMBALI ZA KIMATAIFA pamoja na KITAIFA Endelea kutembelea MTOKA MBALI pia nifuate twitter>>>@mawere3, facebook>>>Mawere Mtoka Mbali, Instagram>>>Zawadi_mawere. SuScribe Youtube>>>MAWERE TV. 

NI NINI MAONI YAKO?



No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...