11 May, 2015

Wanafunzi 'WAPIGWA' Mkutano Ukawa Arusha

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, wanafunzi wa shule za msingi za Mwangaza na Ngarenaro, juzi walidaiwa kupata kipigo kutoka kwa vijana waliojiita ‘Makamanda’ wa umoja wa vyama vya siasa vya upinzani ujulikanao kama Ukawa, baada ya
baadhi yao kufika katika mkutano huo uliofanyika viwanja vya karibu na shule yao.
 
Baadhi ya viongozi wakuu wa umoja huo, akiwemo mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu, Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi) na Mbunge wa Arusha Mjini kwa tiketi ya Chadema, Godbless Lema, walishuhudia kitendo hicho, lakini cha kushangaza hawakuchukua hatua yoyote ya kuwazuia vijana hao kuwachapa watoto mijeledi kwa kisingizio kuwa hawakustahili kuwepo uwanjani hapo.
 
Hatua hiyo imekuja licha ya kuwa umoja huo ulikuwa unafanya mkutano wake katika eneo la shule ya Msingi Ngarenaro, uwanja ambao hutumika na shule za msingi za Ngarenaro na Mwangaza pamoja na shule ya Sekondari ya Ngarenaro.
 
Aidha, wanafunzi hao walikuwa na jukumu la kuotesha majani katika eneo hilo la shule. Katika mkutano huo, viongozi wa Ukawa walidai kuwa uwanja wa shule ya Ngarenaro ulikuwa umelimwa kwa trekta ili kuwazuia kufanya mkutano wao.
 
Hata hivyo, uongozi wa shule ulielezea kuwa katika kipindi cha mvua kama hiki, shule zote za manispaa huwa zinautumia msimu kuboresha mazingira kwa kuotesha majani, maua na miti kutokana na uwepo wa maji ya mvua.
 
Hata wale waliofika kwa ajili ya kusikiliza mkutano, pia walijikuta wakionja joto ya jiwe kutoka kwa ‘Makamanda’ hao. Kipigo cha wanafunzi pia kiliwakera wananchi wengi waliohudhuria mkutano huo na kulaani kitendo hicho.
 
Hata hivyo hakuna mtoto hata mmoja aliyeumia kutokana na sakata hilo, kwani walilazimika kukimbia kutoka uwanjani hapo kuepuka kipigo.
 
Wasemaji wakuu kwenye hadhara hiyo ni pamoja na Lema, Lissu na Kafulila ingawa kwa mujibu wa matangazo yaliyotangulia, kete kubwa ya Ukawa katika kuwakusanya watu ilikuwa ni uwepo wa Lissu.
 

Mawerenewz.blogspot.com ndio mtandao wako wakipekee unaokupa habari za BURUDANI,MICHEZO, SIASA, na HABARI MBALIMBALI ZA KIMATAIFA pamoja na KITAIFA Endelea kutembelea MTOKA MBALI pia nifuate twitter>>>@mawere3, facebook>>>Mawere Mtoka Mbali, Instagram>>>Zawadi_mawere. SuScribe Youtube>>>MAWERE TV.


NI NN MAONI YAKO?
1.

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...