14 May, 2015

JE ULIYAKOSA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI MAY 14,2015? HAYA HAPA

Image result for NEWS DAILY
MWANANCHI
Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Anna Mgwira amesema chama hicho hakina matatizo na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na hata sasa kinasubiri majibu ya barua yao waliyoituma kwa umoja huo kuomba kuunganishwa. Mgwira alitoa kauli hiyo wakati chama hicho kilipofanya
ziara ya kutembelea hospitali ya mkoa ya Mt Meru kugawa zawadi mbalimbali katika wodi ya kinamama ikiwa ni njia ya kuadhimisha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.
Alisema ACT-Wazalendo wanaunga mkono muungano wowote wa vyama vya upinzani nchini ulio halali.
“Hatuna matatizo na Ukawa tunaunga mkono muungano wowote wa upinzani ulio halali,” alisema kiongozi huyo
Alisema tangu waandike barua ya kuomba mwongozo wa namna ya kujiunga na Ukawa, bado hawajapata mrejesho.
“Tunatamani kuunganisha nguvu katika siasa za vyama vya upinzani na sasa tunasubiri majibu ya barua yetu ya kuomba kuingia Ukawa,” .
Alisema kuwa chama hicho kimepokewa vizuri na wananchi wa mikoa mbalimbali nchini na katika ziara ya awamu ya kwanza walifanikiwa kuingiza jumla ya wanachama wapya 700.
Tumepokewa vizuri mikoani tumefanikiwa kuingiza wanachama wapya na hoja ya umoja na uzalendo watu wameipokea vizuri,”  Mgwira.
Akipokea misaada katika hospitali hiyo Muuguzi Mfawidhi, Sifael Masawe alisema kwamba misaada hiyo itasaidia kupunguza shida za wagonjwa.
MWANANCHI
Makada watano wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao ni miongoni mwa wanaotajwa kutaka kuwania nafasi ya urais, wamefanya uamuzi mgumu wa kutangaza kutogombea tena ubunge kwenye majimbo yao.
Wabunge hao na majimbo yao kwenye mabano ni Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta, Waziri Mkuu Mizengo Pinda  na Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowassa .
Wengine ambao wanatajwa kuutaka urais na tayari wametangaza kutogombea tena ubunge ni Spika wa Bunge, Anna Makinda , na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe.
Wakati wabunge hao wakitangaza kuachana na kiti hicho cha uwakilishi, wengine; Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira , Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu wamesema watarudi tena kwenye ubunge kama watashindwa urais.
Mei 26 mwaka 2013, Sitta alikaririwa na vyombo vya habari akisema anafikiria kustaafu ubunge, na tayari ameshawaambia wapigakura wa Urambo Mashariki juu ya azima yake hiyo.
“Viongozi wenzangu msipende kung’ang’ania madaraka. Nawaombeni mjifunze kusema yatosha…staafuni kama ninavyotaka kufanya mimi,” alisema Sitta katika Kongamamo la Mawasiliano katika Nyanja za Digitali la wanafunzi wa Idara ya Uhusiano na Masoko, Chuo Kikuu cha St. Augustine (Saut), Mwanza.
Kwa upande wake, Membe alitoa kauli ya kustaafu ubunge Januari Mosi 2013 kwenye sherehe za Mwaka Mpya nyumbani kwake. Alisema, “Unajua nimekuwa mbunge wenu kwa kipindi cha tatu. Hivi leo ninawaaga rasmi kuwa sitagombea tena nafsi hii ya ubunge.”
Lowassa, amekuwa Mbunge wa Monduli kwa zaidi miaka 20 na kutokana na azma yake ya kutaka kugombea urais,, makada kadhaa wa CCM wameanza kupigana vikumbo kumrithi.
Baadhi ya makada wanaoanza safari ya kumrithi Lowassa Monduli ni aliyewahi kuwa Katibu Uenezi wa CCM Mkoa wa Arusha na Diwani wa Monduli Mjini, Loata Sanare na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Arusha, Namelok Sokoine, ambaye ni mtoto wa Waziri Mkuu wa zamani marehemu Edward Moringe Sokoine.
Pinda ambaye tayari ameshatangaza nia ya kugombea urais alieleza Agosti 17, 2010 kuwa hatagombea tena ubunge katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Pinda aliirudia kauli hiyo katika mkutano wa hadhara jimboni kwake akisema muda wa kuwa mbunge umetosha na sasa anatafuta kitu kingine cha kufanya.
TANZANIADAIMA
Mtoto mchanga wa kiume wa siku tatu katika mtaa wa Masanga Wilaya ya Igunga ameokotwa akiwa amekatwa viungo vyake na watu wasiojulikana.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Masanga Julius Kitundu alisema mtoto huyo aliokotwa na wasamaria wema pembezoni mwa barabara ya lami.
“Kwa kweli kitendo kama hiki kimetusikitisha na watu waliofanya kitendo hicho wanapaswa kusakwa kwa nguvu zote na kufikishwa kwenye vyombo husika” Kitundu.
Mwenyekiti huyo alitoa wito kwa wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi na kuwaomba watoe ushirikiano kwa jeshi la Polisi katika kuwasaka wahusika.
Baadhi ya wananchi wamelaani kitendo hicho cha kinyama na kusema wataanzisha msako mkali ili kuhakikisha waliohusika wanakamatwa na mama aliyejifungua anashikiliwa.
NIPASHE
Kaimu Mtendaji Mkuu wa  Mradi wa Ujenzi wa Barabara ya Mwendokasi jijini Dar es Salaam (Dart), Dk. Asteria Mlambo, amewataka waathirika waliojihifadhi kwenye makalavati ya barabara hizo eneo la Jangwani kuondoka mara moja.
Pia amewaagiza watendaji wa Dart kuwaelimisha na kuwashauri waondoke kwa hiyari kwenye maeneo hayo hadi leo jioni kwani si mahali sahihi pa makazi.
Dk. Mlambo alisema jana kuwa eneo ambalo wakazi hao wamejihifadhi ni kwa ajili ya matumizi ya barabara na siyo makazi hivyo waondoke.
Alisema, watu hao wanaweza kuiharibu miondombinu kwa kuwa haikujengwa kwa ajili ya hifadhi ya watu bali kwa atumizi ya barabara, hivyo shughuli zisizofaa zinazoendelea zitaharibu miundombinu.
“Tayari nimeshawaagiza wafanyakazi wa Dart, waende kuzungumza nao ili waondoke wenyewe kwa hiyari na ifikapo kesho jioni (leo), asionekane mtu yeyote kwenye eneo lile la kituo cha mabasi ya mwendokasi,”Dk. Mlambo.
Alisema wamebaini kuwa wakazi hao ni wale ambao walipewa viwanja eneo la Mabwepande wilayani Kinondoni, lakini hawakutaka kwenda huko na pia wengi wao siyo wenye nyumba bali ni wapangaji.
“Wakazi wa mabondeni serikali inawajali, lakini wenyewe hawajijali, wamepewa maeneo rasmi hawataki kwenda, wamembiwa wahame, lakini hawataki, sasa sijui wanataka nini,” .
Katika eneo hilo, Wafanyakazi wa Kampuni ya Ujenzi wa Barabara hiyo Strabag, wakiendelea na shughuli za kusafisha eneo hilo huku mvua ikiendelea kunyesha.
Rais Jakaya Kikwete, juzi alifika eneo hilo kujionea hali ya mafuriko na  kuwaagiza Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads, kusafisha eneo hilo la daraja kwa kuzoa taka pamoja na mchanga.
Rais Kikwete alisema taka pamoja na mchanga uliojaa katika eneo hilo la daraja ndio unasababisha maji kujaa na kusababisha kupita juu ya daraja badala ya chini ya daraja.
NIPASHE
Serikali imekanusha kuuza eneo la Polisi Oysterbay, jijini Dar es Salaam,  bali imeingia ubia na mwekezaji binafsi ikiwa ni miongoni mwa mikakati ya kupunguza tatizo la nyumba kwa askari.
Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima, wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kasulu Mjini, Mosses Machali, bungeni jana.
Machali alitaka kujua kauli ya serikali kuhusiana na eneo hilo ambalo linadaiwa kuuzwa kupitia Mpango wa Ushirikiano wa Serikali na Sekta binafsi (PPP),  ili yajengwe maduka makubwa.
“Serikali ina kauli gani kuhusiana na jambo hilo wakati inasema kuwa ina mpango wa kujenga nyumba kwa polisi,” alihoji mbunge huyo.
Silama alisema mbia huyo atajenga nyumba za polisi 350 nchini na ameanza kufanya hivyo.
Naye Mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini, alisema katika wilaya ya Rombo nyumba za polisi zimejengwa kwa mabanzi na zina wadudu aina ya kunguni na sungusungu.
Akijibu, Silima alimpiga kijembe  Selasini kuwa ameuliza swali hilo kwa sababu amechangia Sh. milioni 5 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya polisi.
NIPASHE
Mbunge wa Kigoma Mjini (CCM), Peter Serukamba, ameishangaa serikali kumsafisha aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo aliyesimamishwa kazi, Eliakim Maswi, dhidi ya tuhuma za kuhusika katika kashfa ya kampuni ya IPTL ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 200 katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), huku watuhumiwa wengine wakiachwa kusafishwa.
Alisema hayo alipokuwa akichangia hotuba ya mwelekeo wa kazi za serikali, makadirio ya matumizi ya fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Bunge kwa mwaka 2015/16 iliyowasilishwa na Mizengo Pinda, bungeni juzi.
Serukamba alisema inashangaza kusikia kamati iliyochunguza tuhuma dhidi ya Maswi na Prof. Muhongo kwamba, imebaini kuwa ni wasafi na muamala uliofanywa katika akaunti hiyo ulikuwa safi.
Alisema hakubaliani jinsi suala hilo lilivyoshughulikiwa na kutoa taarifa kuwa licha ya suala la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kusimamiwa na wizara hiyo, viongozi wake wanasafishwa kuwa hawana hatia. Alihoji inakuwaje watu wengine wafikishwe mahakamani, waondolewe kwenye nyadhifa na wengine wakiwa bado maofisini.
“…hao ni wachafu? Maswi na Muhongo ndiyo wasafi?Serukamba.
Aliongeza: “Kama wao ni wasafi na muamala wa Escrow ulikuwa safi, kwanini Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka, Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, nao wasisafishwe? au ni wachafu?”
Alimtaka Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, kutangaza kuwa wengine waliotuhumiwa kuwa ni wachafu kama Prof. Tibaijuka, Chenge, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, kuwa nao pia hawana hatia.
Nashangaa wengine wamesafishwa. Mbona William Ngeleja na Victor Mwambalaswa, waliondolewa kwenye nafasi za uenyeviti? Nao wasafishwe,”  Serukamba.
Ngeleja alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala wakati Mwambalaswa alikuwa anaongoza Kamati ya Nishati na Madini. Ngeleja alitajwa kupokea Sh. milioni 40 kutoka kwa mmiliki wa kampuni ya VIP Engineering and Marketing, James Rugemalira, wakati Mwambalaswa alikuwa Mjumbe wa Bodi ya Tanesco iliyotajwa kuhusika katika kashfa ya akaunti hiyo.
Serukamba alitaka Bunge liambiwe kama kuna wasafi, wachafu ni wepi na Katibu Mkuu Kiongozi aeleze usafi wao ni nini?
HABARILEO
Wakuu wa Nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), wamelaani jaribio la mapinduzi ya kumng’oa Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi na kutaka Katiba ya nchi hiyo ifuatwe ili kudumisha amani na utulivu nchini humo.
Aidha, wameagiza mamlaka husika nchini Burundi kutangaza kusimamisha kwa muda uchaguzi mkuu uliokuwa ufanyike Juni 26 mwaka huu ili kurejesha hali ya amani katika nchi hiyo.
Akizungumza jana katika kikao cha ndani kilichofanyika kwa takribani saa nne kutokana na mkutano wa dharura wa wakuu wa nchi za Afrika Mashariki, Mwenyeikiti wa Mkutano huo, Rais Jakaya Kikwete alisema hatua ya kufanya jaribio la mapinduzi halitasaidia kuleta amani katika nchi hiyo.
“Tumekuwa na vikao kwa muda wote tangu asubuhi mpaka muda huu tukijadili suala la Burundi. Tukiwa tunaendelea na vikao kukawa na mambo yanaendelea Bujumbura.
Kama Jumuiya tunalaani mapinduzi ya Burundi na jumuiya inaona kuwa hatua hiyo hataisaidia kumaliza hali ya sasa, hivyo tunataka kuheshimiwa kwa Katiba.
Aliongeza: “Kwa hali iliyopo sasa nchini Burundi, Jumuiya inaona sio mwafaka kufanyika uchaguzi, hivyo tunaziagiza mamlaka husika nchini Burundi kutangaza kuahirishwa kwa uchaguzi huo na ufanyike ndani ya kipindi cha utawala wa uongozi wa sasa kwa muda usiozidi muda wa utawala wa sasa.
Aidha, Kikwete alisema jumuiya itaendelea kuzungumza na wadau wote katika kuhakikisha hali ya amani inarejea ili uchaguzi uweze kufanyika kwa uhuru na haki kwa kuzingatia katiba ya Burundi, sheria ya uchaguzi na kuzingatia maazimio ya Arusha.
“Pia tunalaani vurugu zinazoendelea, hivyo tunavitaka vyama vyote kuhakikisha wanazuia na kuacha vurugu. Jumuiya haitakubali kuona vurugu zinaendelea,” .
Kikwete alisema wakuu wa nchi ya jumuiya hiyo, watakutana baada ya wiki mbili kufuatilia suala hilo na kuchukua hatua stahiki. Hata hivyo, pamoja na Rais Nkurunziza kuwapo nchini jana, hakuweza kufika katika ukumbi wa mkutano Ikulu.
Baadaye jioni ilielezwa Rais Nkurunziza anayeiongoza Burundi tangu Agosti 26, 2005 aliondoka kurejea nchini mwake, lakini habari ambazo zilitufikia wakati tunakwenda mitamboni zinasema rais huyo alishindwa kutua jijini Bujumbura, Burundi na hivyo kurejea tena jijini Dar es Salaam.
Katika mkutano huo, mawaziri wa mambo ya nje na Katibu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk Richard Sezibera walikuwa wa kwanza kuingia katika mkutano huo uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais Kikwete aliingia ukumbini hapo majira ya saa 7.00 mchana ambako alifanya kikao cha ndani na mawaziri wa mambo ya nje wa EAC kwa saa moja kabla ya kuanza kuingia wakuu wa nchi za jumuiya hiyo.
Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta aliwasili ukumbuni hapo saa 8:12 mchana na kufuatiwa na Makamu wa Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, na baadaye Rais wa Rwanda, Paul Kagame na Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ambao walifanya mkutano wa ndani kupitia na kujadili ripoti ya timu ya mawaziri wa mambo ya nje.
Wengine waliokuwamo kwenye kikao hicho, mbali ya Ramaphosa aliyemwakilisha Rais Jacob Zuma, mpatanishi wa mgogoro wa Burundi aliyeachiwa jukumu hilo na aliyekuwa Rais wa Kwanza, Nelson Mandela ambaye naye aliachwa jukumu hilo na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, pia alikuwepo Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AU) na Waziri wa Mambo ya Nje wa Angola ambao ni mwenyekiti Maziwa Makuu.
HABARILEO
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imetangaza bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2015/2016 huku ikiimarisha na kuongeza kodi katika vyanzo vya mapato kutokana na washiriki wa maendeleo kupunguza misaada yao ya kibajeti.
Waziri wa Fedha na Uchumi, Omar Yussuf Mzee alisema hayo wakati akiwasilisha bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2015/2016 ambapo Serikali inatarajiwa kutumia jumla ya Sh bilioni 830.4.
Alisema fedha zinazotokana na washirika wa maendeleo zimepungua na hivyo kudhoofisha mipango ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na Serikali imeweka zaidi mikakati yake ya kubuni vyanzo vipya pamoja na kuziba mianya yote iliyokuwa ikivujisha mapato.
Aliziita, baadhi ya mikakati ya vyanzo vya mapato ambavyo vitaimarishwa kuanzia sasa na wananchi kutozwa kodi ni pamoja na ada ya usajili wa ardhi na upimaji.
Alisema maeneo mengi Zanzibar hayajapimwa pamoja na kufanyiwa usajili na hivyo kulikosesha taifa fedha nyingi ambapo katika kuweka mikakati ya usajili wa ardhi kwa mwaka zaidi ya Sh bilioni 262 zinatarajiwa kupatikana.
Katika bajeti hiyo, Waziri wa Fedha ametangaza kuwepo kwa ongezeko la kodi katika viwanja vya ndege pamoja na bandari za Unguja na Pemba kwa kiwango cha ongezeko la ada Sh 2,000.
Kwa upande wa abiria wanaofanya safari za kwenda Tanzania Bara watalazimika kulipa ada ya bandari Sh 2,000 pamoja na ada kwa upande wa viwanja vya ndege ambapo maeneo yote hayo yataiwezesha Serikali kujipatia jumla ya Sh bilioni 280.
Alisema bodi ya mapato (ZRB) inatarajiwa kukusanya jumla ya Sh bilioni 225.7, wakati TRA inatarajiwa kukusanya jumla ya Sh bilioni 175.
Aidha alisema Serikali ya Mapinduzi inatarajiwa kuingiza jumla ya Sh bilioni 21, ikiwa ni fedha zinazokusanywa kutoka kwa watumishi wa Serikali ya Muungano waliopo Zanzibar kutokana na makato yanayotokana na makusanyo ya mishahara.
Mzee alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mwaka 2015/2016 imeweka kipaumbele utekelezaji wa bajeti katika sekta ya miundombinu na ujenzi wa viwanja vya ndege pamoja na maji safi na salama kwa asilimia 53.2.
Alisema katika eneo hilo la mawasiliano serikali inatazamiwa kutumia jumla ya Sh bilioni 212 kwa ajili ya kazi hizo ambazo zitakapotekelezwa kwa kiasi kikubwa zitasaidia kupiga hatua kubwa ya maendeleo.
Aidha, sekta ya elimu alisema imetengewa jumla ya Sh bilioni 120.7 na huku kipaumbele, ikiwa ni kuhakikisha kwamba sekta ya elimu inapata mafanikio ambapo Serikali imefuta michango yote iliyokuwa wakitozwa wazazi kutoka kwa wanafunzi.
 “Kuanzia mwaka wa fedha 2015/2016 tunafuta malipo yote ya ada waliyokuwa wakitozwa wazazi na sasa michango yote inafutwa na Serikali inabeba jukumu hilo,” alisema.
RAIA TANZANIA
Jeshi la Polisi Mkoani Simiyu linamshikilia Mwenyekiti wa kijiji cha Bukigi kupitia chama cha Mapinduzi CCM  kwa kosa la kukutwa na viungo vya binadamu likiwemo fuvu la kichwa na mifupa.
Mtuhumiwa huyo ambaye pia ni mganga wa jadi alikamatwa nyumbani kwake baada ya kuwepo kwa taarifa kuwa amewahifadhi majambazi wakisubiri kupangwa waendelee na uhalifu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu Gemin Mushy alisema tukio hilo lilitokea Mei 9 na walipata taarifa kutoka kwa wasamaria wema.
Alisema kuwa upepelezi unaendelea kubaini iwapo kweli viungo hivyo ni vya binadamu na kama kuna watu wengine wanahusika.
UHURU
Ikulu ya Tanzania sio mahali pa kuishi wagonjwa na watu waliochoka, bali ni kwa ajili ya viongozi makini na shupavu na wenye uwezo wa kuliongoza Taifa.
Imeelezwa kuwa viongozi waliochoka kama katibu wa Chadema Wilbroad Slaa ambaye amekuwa akipigiwa chapuo kuwania Urais hana sifa za kuishi ikulu.
Mbunge wa Mtera Livingstone Lusinde alisema  viongozi wa Chadema akiwemo muhasisi wake Edwin Mtei wamechoka na licha ya kuchoka pia wamekuwa tegemeo ndani ya CHADEMA na ndio sababu wamekuwa wakipigiwa upatu kuingia ikulu.
Lusinde alikiri kuwa Serikali ya CCM imechoka kutokana na kufanya kazi nyingi za kuwatumikia wananchi wake kwa kutumia akili nyingi,maarifa na nguvu kwa lengo la kuhakikisha wanaishi katika maisha mazuri.
Alisema Serikali imekuwa ikitekeleza mambo menfi ya maendeleo kwa wananchi wake huku ikitimiza ahadi zote ilizoahidi katika ilani ya Uchaguzi tofauti na wapinzani.

Mawerenewz.blogspot.com ndio mtandao wako wakipekee unaokupa habari za BURUDANI,MICHEZO, SIASA, na HABARI MBALIMBALI ZA KIMATAIFA pamoja na KITAIFA Endelea kutembelea MTOKA MBALI pia nifuate twitter>>>@mawere3, facebook>>>Mawere Mtoka Mbali, Instagram>>>mawere_mtoka_mbali,SuScribe Youtube>>>MAWERE TV



No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...