18 May, 2015

Huu ndio Muda wakuyapitia magazeti ya leo MAY19,2015 KAMA HAUKUPATA NUDA WAKUYAPITIA LEO

ILOOOMWANANCHI
Mhasibu wa Hospitali ya Rufaa KCMC, Paul Mhumba amesimamishwa kazi kwa tuhuma za kutuma ujumbe wa simu ya mkononi (sms) kwa Rais Jakaya Kikwete.Kuvuja kwa ujumbe huo na nambari ya simu iliyotuma, kumeibua hisia tofauti kuhusu usiri wa ofisi ya Rais katika
kushughulikia malalamiko nyeti ya wananchi na kuwaweka njiapanda watoa habari za siri.
Mhumba, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Afya na Serikali Kuu (TUGHE) Tawi la KCMC anadaiwa  na Menejimenti ya KCMC kuwa ndiye aliyetuma ujumbe huo.
Katika barua yake ya Mei 5, ilidai uchunguzi umebaini kuwa Mhumba ndiye mtumaji wa ujumbe huo.
“Uongozi umepokea taarifa iliyotumwa mwishoni mwa Aprili na mwanzoni mwa Mei mwaka huu kwa njia ya ujumbe wa simu kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Jakaya Kikwete,” .
KCMC imedai katika barua hiyo, taarifa hiyo ya sms ilibeba ujumbe unaohusiana na matumizi mabaya ya fedha za hospitali hiyo unaofanywa na baadhi ya viongozi na Shirika la Msamaria Mwema (GSF).
Mbali na tuhuma hizo, lakini pia KCMC inadai taarifa hiyo ilimweleza Rais kuwa KCMC na GSF linalomiliki hospitali hiyo, zinajitosheleza kwa mapato, hivyo hakuna haja kwa Serikali kuendelea kuipatia ruzuku.
Pia, menejimenti imedai taarifa hiyo ilidai wafanyakazi wa KCMC wanatumikishwa kama watumwa, hivyo ni maombi yao (watumishi) Serikali ilegeze masharti ili ajira zao zichukuliwe na Serikali.
MWANANCHI
 Chama cha NCCR-Mageuzi kimeponda kauli ya Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu kwamba Katibu mkuu wa chama hicho kikuu cha upinzani, Dk Willibrod Slaa ndiye atakayekuwa mgombea urais kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
Akiwa kwenye mkutano wa hadhara wa Chadema mjini Moshi, hivi karibuni, Lissu alikaririwa akieleza kuwa Dk Slaa, ndiye atakayepitishwa na Ukawa kugombea nafasi hiyo.
Lakini Mkuu wa Idara ya Kampeni na Uchaguzi wa NCCR-Mageuzi, Faustine Sungura aliliambia gazeti hili mwishoni mwa juma kuwa ni makosa kudhani kwamba Chadema ndicho chenye nafasi ya kusimamisha mgombea urais kupitia Ukawa, wakati bado mchakato wa kumpata mgombea haujafanyika.
Sungura ambaye pia ni miongoni mwa waasisi na mwanzilishi wa mageuzi nchini, alisema kati ya vyama vinne vilivyounda Ukawa, tayari Chadema imepewa majimbo mengi ya ubunge. “Fursa hiyo pekee imeshawapa uwezekano wa kutoa waziri mkuu kama upinzani utashinda”, alisema.
“Kwa kawaida chama chenye wabunge wengi ndicho kinachotoa waziri mkuu, sasa kwa namna yoyote Chadema ndiyo itakayotoa waziri mkuu, hivyo haiwezekani watoe na mgombea urais. Nawashauri wachague nafasi mojawapo,”  Sungura.
Sungura alisema kauli hiyo ya Lissu siyo sahihi na hailengi kujenga Ukawa, bali kuubomoa kwa kuwa haiwezekani chama kimoja kitoe rais, makamu wake na waziri mkuu. “Ni vizuri ikaeleweka mapema kwamba, haiwezekani chama kimoja kati ya vyama vinne washirika wa Ukawa, kikatoa mgombea urais, makamu na waziri mkuu,” alisema Sungura  na kuongeza:
“Kwa kuwa CUF kina nafasi kubwa ya kumtoa mgombea urais wa Zanzibar, vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema na NLD, kimoja kati ya vyama hivyo kitamtoa ama rais au waziri mkuu au spika wa Bunge, kinyume chake ni tamaa inayoweza kuua Ukawa.
MWANANCHI
Wakati uandikishaji wapigakura ukiendelea kulalamikiwa katika Mkoa wa Lindi kutokana na kasoro mbalimbali, madudu zaidi yamebainika, huku Chama cha Wananchi (CUF) kikiitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuweka hadharani idadi ya watu wanaoandikishwa katika kila kata.
Miongoni mwa kasoro zinazolalamikiwa ni pamoja na vituo vya kujiandikisha kuwa tofauti na vile vya kupigia kura na mashine za Biometric Voter Registration (BVR) kuondolewa kabla ya watu kujiandikisha.
Mwenyekiti wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba alisema jana kuwa idadi ya watu waliondikishwa katika kila kata ikiwekwa wazi na NEC itawasaidia kulinganisha na makadirio ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ili kufahamu idadi ya watu wasioandikishwa.
Alisema viongozi wa chama hicho walifanya ziara mikoa Ruvuma, Lindi na Mtwara na kushuhudia kasoro nyingi katika uandikishaji.
Akitoa mfano, alisema katika Kata ya Matemanga wilayani Tunduru, asilimia 60 ya watu wenye haki ya kupiga kura hawajaandikishwa, lakini mashine zimehamishwa.
Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva alisema kila aliyefika kwenye kituo cha kuandikisha aliandikishwa.
Niko Mtwara kutembelea vituo, ninachoweza kusema ni kwamba tume haimfuati mtu nyumbani kwake kwenda kumwandikisha, kila aliyefika kituoni aliandikishwa, sehemu zote tunazopita hakuna malalamiko, sijui akina Lipumba wanapata wapi taarifa hizo, mambo mengine siwezi kuyazungumza kwa sasa,” alisema.
NIPASHE
Baadhi ya wabunge wamemtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuwa mkweli kuhusu kuwasafisha viongozi watuhumiwa wa Escrow na Operesheni Tokomeza, badala ya ‘kuhadaa’ kuwa wanaendelea kuchunguzwa.
Waziri Mkuu akihitimisha mjadala wa bajeti yake juzi mjini Dodoma, alisema Ikulu haijawasafisha viongozi hao kwa vile wanaendelea kuchunguzwa.
Akichambua maelezo ya Pinda, Mbunge wa Muhambwe (NCCR-Mageuzi), Felix Mkosamali, alisema Watanzania wanatakiwa kumshangaa kiongozi huyo kwa kutolieleza taifa ukweli.
Waliosafishwa na Ikulu ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi na aliyekuwa waziri wa wizara hiyo, Prof. Sospeter Muhongo.
Wengine ni mawaziri waliowajibika kutokana na kashfa ya Tokomeza, Dk. Emmanuel Nchimbi,  Balozi Khamis Kagasheki na Shamsi Vuai Nahodha .
Wabunge hao waliwajibishwa na Bunge kwa kushindwa kusimamia operesheni hiyo na kutaka wawajibike kwani ilisababisha vifo, udhalilishaji, mateso kwa watu na uharibifu wa mali.
Mwingine aliyelazimika kujiuzulu katika sakata hilo ni Dk. David Mathayo David, ingawa Bunge halikumuwajibisha.
Mkosamali alisema Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma, vyote viko chini ya Ofisi ya Rais, haviwezi kufanya kazi kwa kupingana.
Alisema Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, alitoa taarifa ya kamati ya uchunguzi kwa niaba ya Rais, hivyo kusema kuwa kuna taasisi nyingine ndani ya Ikulu zinaendelea na uchunguzi, ni jambo la kushangaza.
“Tungeelezwa na Ikulu maoni na mapendekezo ya Sekretarieti ya Maadili, kwa vile hatujaambiwa kilichoko kwenye ripoti yake. Lakini Sefue pia awafahamishe wananchi, hicho alisema ni cha Kamati ya Rais na ya Makatibu Wakuu, mapendekezo ya sekretarieti hiyo yako wapi?”
Mkosamali alishauri kuwa kwa vile hizi ni zama za uwazi, sheria zifanyiwe marekebisho ili zitoe muda maalum kwa Rais kutangaza ripoti na mapendekezo ya sekreterieti ili kuongeza uwazi.
Mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema, alisema wamesafishwa kwa vile anachosema Sefue ndizo taarifa za Ikulu.
Ukisema hajawasafisha unategemea nani mwingine azungumzie habari na ripoti za tume hizo zilizoteuliwa na Rais na kupeleka mapendekezo Ikulu. “Ni Sefue ndiye Ikulu na Ikulu ndiyo yeye,” alisema.
Alisema Maswi amesafishwa kwa kuwa ndiye aliyeandika barua fedha zitolewe kutoka Benki Kuu (BoT), ukisema anachunguzwa zaidi na nani mbona kila kitu alichofanya kinafahamika? Ikulu inawafahamu wote waliochota fedha kwenye Benki ya Stanbic na kwingineko mbona hawajatajwa?” alihoji na kuendelea:
“Kusema wanaendelea kuchunguzwa ni mchezo wa kisiasa na kufunika kombe mwanaharamu apite au kumaliza mambo kimya kimya.”
HABARILEO
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) inatarajia kusambaza vijana wa kazi katika majimbo yote nchini, kuwashughulikia wote walioonesha nia ya kugombea nafasi mbalimbali za uchaguzi, ambao wanatoa rushwa ili kupata wafuasi.
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hosea, alisema hayo jana alipokuwa akijibu agizo alilopewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, George Mkuchika katika semina ya wabunge wa Mtandao wa Wabunge wa Afrika wa Kupambana na Rushwa (APNAC), tawi la Tanzania.
Mkuchika alimtaka Dk Hosea asisubiri kipenga cha kampeni kuanza, bali asambaze vijana wake kwenye majimbo ya uchaguzi kwani viashiria vya rushwa vimeshaanza.
Kazi imeanza, waambie vijana wako wasisubiri Oktoba, waanze kazi sasa maana kuna viashiria vya rushwa, waingie wafanye kazi,Mkuchika.
Alisema semina hiyo imekuja wakati mzuri wanapoelekea kwenye Uchaguzi Mkuu Oktoba mwaka huu, hivyo ni vyema wabunge wakumbuke wana wajibu wa kulinda maadili na kuepuka vitendo vya rushwa.
Akijibu hoja mbalimbali za wabunge baada ya kuwasilisha mada ya rushwa na uchaguzi, Dk Hosea alizungumzia hatua zitakazochukuliwa na Takukuru kwa watoa rushwa kupitia njia ya mtandao, ambapo alisema kwa uchaguzi huu ni vyema watoa rushwa kwa njia hiyo waache.
Katika swali lake, Mbunge wa Nkasi, Ali Keissy (CCM), alihoji njia zitakazotumika kubaini wanaotumia njia ya mtandao kutoa rushwa, ambapo Dk Hosea alisema wanajua hilo na watalifuatilia kwa kuwa wana uwezo wa kufanya hivyo.
Dk Hosea alisema miamala yote inayofanywa na wagombea itafuatiliwa na kutoa rai kwa wagombea kuacha kutoa rushwa, kwani watakaobainika sheria itachukua mkondo wake.
“Nyie mnaotumia mitandao ya simu kutoa rushwa, mwaka huu mtaumia vibaya acheni, tuna uwezo wa kudhibiti vitendo hivyo, tumesomesha vijana wetu na tuna vifaa vya kufuatilia,”Dk Hosea.
Alisema uchaguzi wa mwaka huu utakuwa tofauti na wa mwaka 2010, kwani wamejipanga vizuri kuhakikisha vitendo vya rushwa vinadhibitiwa.
Moja ya mbinu zitakazotumika kwa mujibu wa Dk Hosea, ni kubadilisha magari yao yanayotumika kwenye uchunguzi kwa kuwa yaliyopo yameshazoeleka.
“Niwaambie tu tutatumia magari mengine maana haya ya sasa mmeyazoea, mnayajua na wengine walinunua yanayofanana ili iwe rahisi kwao kutoa rushwa wakiwa ndani…sasa watu hawatayatambua kama ni ya kwetu au la,Dk Hosea.
Akijibu swali la Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM), aliyehoji kusafishwa kwa baadhi ya watuhumiwa wa sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow kama hakuharibu uchunguzi wa Takukuru, Dk Hosea alisema hakuna kilichoharibika.
“Sisi hatusafishi mtu na mafaili yetu hatujayafunga na wala hatuna mpango wa kuyafunga, tunafanya kazi kwa mujibu wa sheria na kazi yetu ya kuwachunguza inaendelea na tukimaliza tutakabidhi kwa mamlaka nyingine,”  Dk Hosea.
Alisema kusafishwa kwa baadhi ya watuhumiwa wa tukio hilo hakujaharibu uchunguzi wao na kwamba wao wanaendelea na kazi yao na hakuna aliyewaingilia kwenye kazi yao, hivyo watahakikisha wanaikamilisha.
HABARILEO
Mtoto wa kike mwenye umri wa miaka tisa ameonesha ujasiri wa kipekee kwa kumwokoa mama yake mzazi, Magreth Ibrahim (50) kuuawa na mamba baada ya kupambana na mnyama huyo kwa zaidi ya nusu saa.
Mama huyo mkazi wa kijiji cha Karema, mwambao mwa Ziwa Tanganyika wilayani Mpanda, kwa sasa amelazwa katika Hospitali ya wilaya ya Mpanda mjini Mpanda kwa matibabu baada ya mkono wake kunyofolewa na mamba aliyemshambulia wakati akifua kando ya Mto Ikola.
Akimweleza Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, Paza Mwamlima aliyemtembelea hospitalini hapo masaibu yaliyomsibu, alisema anamshukuru sana binti yake mwenye umri wa miaka tisa aliyeweza kuokoa maisha yake licha ya kuwa amenyofolewa mkono na mamba huyo.
Akisimulia mkasa huo, Magreth alieleza kuwa juzi akiwa anafua kando ya mto Ikola ghafla mnyama huyo aliibuka majini na kumpiga usoni na mkia wake.
“Mamba huyo aliibuka ghafla mtoni na kunichapa usoni na mkia wake nami nikaangukia majini ndipo aliponidaka mkono wangu na kunivutia mtoni ….binti yangu aliyekuwa jirani yangu alipoona niko karibu kuliwa na mamba kwa ujasiri aliweza kukabiliana naye … Alinishika mkono mwingine na kunivutia nje huku akipiga kelele kumtisha mnyama huyo ili aniachie hatimaye akaunyofoa mkono wangu na kutokomea nao mtoni ….” alieleza.
Aliongeza kuwa watu waliokuwa wakifua mtoni hapo wengi wao wakiwa wanawake walifika eneo la tukio ambapo wakiwa na binti yangu walimvuta na kumtoa nje na baadae wakamkimbiza hospitalini mjini Mpanda kwa matibabu.
Naye Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, Dk Joseph Mkemwa amethibitisha kuwa hali ya mama huyo inaendelea kuimarika baada ya kupatiwa matibabu.
HABARILEO
Raia wa Tanzania na Msumbiji watakaotaka kuingia katika nchi hizo na kukaa wa miezi isiyozidi mitatu, hawatalipia viza kama ilivyokuwa awali, imeelezwa.
Aidha, imetangazwa pia kuwa, wanafunzi kutoka katika nchi hizo kuanzia sasa wanaruhusiwa kusoma kokote ndani ya Msumbiji na Tanzania wakitumia pasipoti zao zitakazogongwa viza bure, kwa kipindi chote cha masomo yao, hata kama ni miaka mingi.
Hatua hizo zimefikiwa Ikulu, Dar es Salaam jana baada ya Marais Jakaya Kikwete na Filipe Nyussi wa Msumbiji kukubaliana kufanyia marekebisho mkataba wa masuala ya uhamiaji kati ya nchi hizo mbili kudumisha udugu, urafiki na uhusiano wa kirafiki.
Makubaliano hayo yalifikiwa baada ya viongozi hao wakuu wa nchi hizo kufanya mazungumzo ya faragha kwa saa kadhaa Ikulu, na kisha Mawaziri Jaime Basilio Monteiro, wa Mambo ya Ndani wa Msumbiji na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania, Bernard Membe, aliyemwakilisha Waziri wa Mambo ya ndani ya nchi, Mathias Chikawe, kusaini hati ya makubaliano hayo.
Mkataba huo wa sasa wenye marekebisho katika maeneo matatu makuu, umeeleza pia kuwa muda wa siku 30 uliokuwa ukitolewa na Msumbiji kwa watanzania, kukaa nchini humo bila kulipia viza sasa umeongezwa na kuwa siku 90.
Kutokana na matakwa mapya ya mkataba huo wa sasa, Membe alisema umeweka usawa wa siku za kuishi kwenye nchi hizo mbili kwa raia wa Tanzania na Msumbiji, tofauti na ilivyokuwa awali kwamba watanzania walipewa siku hizo kuwepo bure kwenye nchi hiyo wakati raia wa Msumbiji waliweza kuishi kwa siku 90 bila kutozwa ada ya viza.
“Makubaliano ya Marais hawa yameleta ahueni kubwa kwa raia wa nchi hizi mbili katika masuala ya uhamiaji. Wanafunzi nao wamepata nafuu kubwa kwa sababu hawataulizwa ada ya viza tena hadi wamalize masomo,”  Membe.
Aliongeza kuwa, mabadiliko hayo yanahusu hati za kidiplomasia, za kiserikali na za kawaida ambapo, mtumiaji atagongewa viza bure kwa siku atakazo kaa, ilimradi zisizidi 90.
Membe alieleza kuwa kabla ya makubaliano hayo, raia wa Msumbiji alipaswa kulipa ada ya viza ya Sh 10,000 tu, ili kukaa nchini kwa siku zisizo zidi 90, wakati raia wa Tanzania aliyekwenda Msumbiji na kukaa kwa zaidi ya siku 30, alipaswa kulipa Dola za Marekani 900 ikiwa ni ada ya viza.
Pia,Mtanzania aliyekwenda nchini humo kwa shughuli za biashara alipaswa kulipa ada ya viza ya Dola za Marekani 700, wakati mfanyabiashara wa Msumbiji aliyekuja nchini kwa shughuli kama hizo alitozwa ada ya viza ya Dola za Marekani 200 tu.

Mawerenewz.blogspot.com ndio mtandao wako wakipekee unaokupa habari za BURUDANI,MICHEZO, SIASA, na HABARI MBALIMBALI ZA KIMATAIFA pamoja na KITAIFA Endelea kutembelea MTOKA MBALI pia nifuate twitter>>>@mawere3, facebook>>>Mawere Mtoka Mbali, Instagram>>>mawere_mtoka_mbali,SuScribe Youtube>>>MAWERE TV

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...