21 April, 2015

Masharti ya ZITTO aliyoyatoa kwa LOWASSA ili kujiunga ACT na Mtoto wa miaka 11 ajinyonga Dar…Ni miongoni mwa stori 9 #MAGAZETINI APRIL 21

WWWMWANANCHI
Kiongozi wa Chama cha ACT – Wazalendo, Zitto Kabwe amesema iwapo Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa anataka kugombea urais kupitia chama hicho afuate taratibu za chama ikiwamo kutangaza mali zake.
Akiwahutubia mamia ya
wakazi wa Jiji la Mwanza kwenye Viwanja vya Furahisha juzi, Zitto alisema hawezi kumzuia mtu anayetaka kujiunga ACT – Wazalendo ikiwa atafuata taratibu zilizowekwa na chama hicho.
“Naomba niwaambie Watanzania kwamba ACT siyo chama cha kumtengenezea mtu mazingira ili agombee urais, lakini kama Lowassa anataka kugombea urais kupitia huku lazima atangaze mali zake na kueleza wapi amezipata kama taratibu za chama zinavyosema,”  Zitto.
Zimekuwapo taarifa kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kuwa baadhi ya wagombea akiwamo Lowassa ambaye anatajwa kuwania urais kupitia CCM, wana mpango wa kutimkia ACT iwapo watakatwa majina yao katika mchujo wa wagombea.
Kwa mujibu wa habari hizo, ACT – Wazalendo imepewa fedha na Lowassa ambazo inatumia katika mikutano hiyo kumwandalia nafasi ya kuwania urais, madai ambayo pande zote zimeyakanusha.
Akizungumzia taarifa hizo kwenye mkutano huo, Zitto alisema chama chake kinaongozwa kwa kufuata taratibu na kitampokea yeyote atakayefuata taratibu hizo.
Kiongozi huyo ambaye hivi karibuni alitangaza mali na madeni yake, alisema iwapo Lowassa atataka kujiunga na chama hicho itambidi atangaze mali zake na kueleza jinsi alivyozipata, kama yeye alivyofanya.
Hata hivyo, akizungumzia kuhusu kauli ya Zitto, msemaji wa Lowassa, Aboubakary Liongo alisema: “Hakipo kitu kama hicho na hakitakuwapo, hatujui habari hii inatoka wapi? Mzee (Lowassa) amekuwa akitumikia CCM maisha yake yote tangu enzi za TANU … yupo na anaendelea kutumikia kifungo chake. Maisha yake yote ni mtumishi wa chama.”
Lowassa pamoja na makada wengine watano wa chama hicho walipewa adhabu ya onyo kali baada ya Kamati Kuu ya CCM kuwatia hatiani kwa kuanza kampeni za urais mapema na kukiuka maadili ya chama.
MWANANCHI
Kamati Kuu ya Chama cha Tanzania Labour (TLP), imempendekeza Mwenyekiti wa chama hicho, Augustine Mrema kutetea kiti chake cha ubunge katika jimbo la Vunjo.
Kaimu Katibu Mkuu wa TLP Nancy Mrikaria, alisema  jana kuwa kamati hiyo pia imemthibitisha Mrema kuendelea na nafasi yake ya uenyekiti wa chama hicho kwa kipindi kingine.
Alisema kamati imeridhia Mrema kuendelea kugombea ubunge katika jumbo la Vunjo ikiwa na imani kuwa ana nafasi kubwa ya kushinda, ikilinganishwa na wengine watakaojitokeza kupambana nao.
“Kamati imefikia hatua hiyo kwa kutambua uwezo alionao mwenyekiti katika kukiendeleza chama, pia hadi sasa hakuna mwanachama mwingine aliyejitokeza kugombea nafasi hiyo na tulianza kutoa fomu tangu Aprili 9 hadi 17, wakati kwenye nafasi ya makamu mwenyekiti Bara ndiyo kuna ushindani wa watu wawili wanaoigombea,”Mrikaria
Alisema nafasi ya Makamu Mwenyekiti upande wa Zanzibar pia haina mpinzani kwa kuwa hadi sasa aliyechukua fomu ni Alhaji Hamad Mkadam ambaye ndiyo anashika nafasi hiyo.
“ Tunatarajia wajumbe wa mkutano watajitokeza kwa wingi ili kufanikisha uchaguzi huo ambao ni muhimu kwa maendeleo ya chama, hasa katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi mkuu kwa kuwa ukikamilika tunapata nafasi ya kujipanga,” Mrikaria.
Naye Mrema alisema kwamba anaamini kwamba kamati hiyo imempendekeza kutokana na kuwa na imani naye kwamba ana uwezo mzuri wa kukiendeleza chama hicho.
“ Siyo kwamba nitakuwa nagombea kwa ubabe au ujeuri bali kamati yenyewe imenibariki, naamini Vunjo nitashinda na kuendelea kukifanya chama kistawi kwani nisipokitetea chama kitakuwa kama cha wacheza ngoma,” Mrema.
Hadi kufikia hatua hiyo ya kufanya uchaguzi TLP ilibanwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, kwa kupewa siku 80 kwa uongozi kuhakikisha kinafanya uchaguzi wake wa ndani ili kuwapata viongozi wapya.
MWANANCHI
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), kimeshika nafasi ya kumi miongoni mwa vyuo vikuu 50 bora na vyenye umaarufu Afrika.
Kadhalika UDSM kimetajwa kuwa miongoni mwa chuo vikuu chenye idadi kubwa ya wanafunzi na walimu na wingi wa programu za masomo.
Makamu Mkuu wa chuo hicho, Prof. Rwekaza Mukandala alisema chuo hicho kina haki ya kushika nafasi hiyo kutokana na jitihada zinazofanywa na uongozi.
“Tulifanya jitihada kuhakikisha tuna walimu wazuri wenye shahada za uzamili na uzamivu, maabara nzuri na miundombinu rafiki ya kufundishia,” Mukandala.
Alisema UDSM ina mitaala bora inayoendana na wakati na inazalisha wataalamu wengi kwa mwaka.
Katika matokeo ya utafiti huo uliofanywa na Taasisi ya Kimataifa ya Vyuo Vikuu na vya Kati (4ICU) ya Uingereza, chuo hicho kilishika nafasi ya 10 kati ya vyuo 50 vilivyopimwa kulingana na vigezo vya taasisi hiyo.
Hata hivyo, taasisi hiyo ilieleza kuwa hawapimi ubora wa vyuo kwa kuangalia kiwango cha elimu inayotolewa au huduma bali wanaangalia umaarufu wa chuo kimataifa.
Katika taarifa hiyo, Chuo Kikuu cha Cape Town cha Afrika Kusini kilishika nafasi ya kwanza huku vingine vilivyoshika tano bora vikitoka nchini humo.
Nafasi ya pili ilishikwa na Chuo Kikuu cha Pretoria, ya tatu Chuo Kikuu cha Stellenbosch na nne ilikwenda kwa Chuo Kikuu cha Witwatersand na tano ikishikwa na Chuo Kikuu cha Afrika Kusini.
MWANANCHI
 Kuna kila dalili kuwa wanasiasa nchini wamebuni mbinu mpya ya kuzitumia klabu za mbio za pole maarufu kama ‘jogging’ kutekeleza mikakati ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu, mwaka huu.
Wachambuzi wa masuala ya kisiasa na baadhi ya wananchi walisema kuwa matukio ya kijamii yanayoendelea hivi sasa nchini na kuhusisha wanasiasa yanapaswa kutazamwa kwa jicho la karibu.
Juzi kulikuwa na matukio makubwa mawili katika maeneo tofauti jijini hapa yaliyohusisha matembezi ya kilomita kadhaa yaliyokuwa yakifanya kampeni mbili tofauti na kuhusisha vigogo wa ngazi ya juu wa CCM.
Katika tukio la kwanza, vijana wapatao 10,000 kutoka klabu mbalimbali za mbio za pole wakiongozwa na wenyeji wao Temeke Family, walimwalika Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa kuongoza matembezi ya kulaani na kupinga ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino).
Lowassa katika tukio hilo aliambatana na wabunge Idd Azzan, Mussa Zungu na Abbas Mtemvu aliyekuwa mwenyeji wa matembezi hayo yaliyoanzia Uwanja wa Taifa hadi Viwanja vya TCC Chang’ombe.
Katika upande mwingine, jimboni Segerea, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akiongozana na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye waliongoza klabu 100 za ‘jogging’ kuhamasisha vijana wajiandikishe katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Wakati wa kuanza hotuba yake, Lowassa alisema hawezi kuzungumza kwa kirefu kutokana na kifungo kinachomkabili cha kutumikia adhabu ya kuanza kampeni za urais mapema alichopewa na chama chake.
Mhadhiri wa Sayansi ya Siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Richard Mbunda alisema kipindi kama hiki wanasiasa hutumia kila mbinu ya kuongeza ushawishi kwa wapiga kura, hivyo matumizi ya klabu za mbio za pole ni moja ya njia za kukuza umaarufu wao.
“Kitendo cha mwanasiasa kushiriki kwenye klabu za ‘jogging’ kinatengeneza ngome ya umaarufu, ataonekana na kuandikwa kwenye vyombo vya habari. Siasa ni vita. Wapo wengine wanatumia hadi njia za kuandika vitabu ili jamii iwakubali,” Mbunda.
Alisema matukio yoyote yanayoendelea na kuhusisha wanasiasa yasipuuzwe licha ya mengine kugusa masuala ya kijamii ambayo ni vigumu mtu kuyang’amua kuwa yanahusisha siasa.
NIPASHE
Wakati serikali ikitangaza kuwarejesha Watanzania 21 kati ya 23 walioko kwenye moja ya makambi yanayowahifadhi raia wa kigeni walioathirika na vurugu zilizohusisha mauaji, uporaji na watu kukimbia makazi nchini Afrika Kusini, Mtanzania aliyeko nchini humo, amesimulia jinsi raia wengi wa kigeni walivyoathirika.
Joseph Moses, anayeishi mjini Durban, amesema pamoja na baadhi ya raia wa kigeni kuawa, lakini waliothirika hadi sasa wengi wao hawajui watalipwaje mali zao zilizopotea katika ghasia hizo.
Moses, alisema kuna Watanzania wengi mjini Durban wamepoteza mali zao katika vurugu hizo na hawajui watalipwaje.
Hata hivyo, alisema raia wa kigeni walioathirika zaidi na ghasia hizo ni wanaotoka katika nchi za China, Pakistan, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Nigeria na Somalia, baada ya maduka pamoja na nyumba wanazoishi kuvamiwa na watu wanaosaidikiwa kuwa ni raia wa Afrika Kusini na kuporwa.
Kinacholeta utata ni kwamba, hata kama fidia itatolewa haijulikani itakuwaje,”  Moses na kuongeza kuwa kuna idadi kubwa ya Watanzania wanaoishi katika mji wa Durban ambao umeathiriwa zaidi na vurugu hizo.
Alisema jana ulifanyika mkutano uliomhusisha Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma, Chifu wa Wazulu, Goodwill Zweluthini anayetuhumiwa kuchochea vurugu hizo na viongozi wengine nchini humo katika kambi ya waathirika hao  mjini Durban.
Moses alisema katika mkutano huo, Chifu Zweluthini aliwapiga marufuku raia wa Afrika Kusini kuendelea kuwashambulia raia wa kigeni.
Alisema sababu iliyotolewa na Chifu Zweluthini ni kwamba, nchi nyingi za Afrika, ikiwamo Tanzania, ziliwasaidia weusi wa nchi hiyo kuondoa siasa ya ubaguzi wa rangi.
Wakati Moses akisema hayo, Watanzania 21 kati ya 23 walioko kwenye kambi hiyo wamekubali kurejea nchini baada ya serikali kuwahakikishia kuwalipia gharama za safari, lakini wawili wamekataa.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, aliwaambia waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam kuwa, Watanzania wanaoishi Afrika Kusini wanakisiwa kuwa zaidi ya 10,000.
Alisema kati yao, 23 ndio waliobainika kuhifadhiwa katika kambi hiyo kufuatia kuibuka kwa ghasia hizo nchini humo.
Kutokana na hali hiyo, alisema serikali imekubali kugharimia safari ya Watanzania hao 21 baada ya wenyewe kukubali kurejea nchini.
Alisema Watanzania hao 21 ni miongoni mwa raia wa kigeni ambao baadhi wanasadikiwa kupoteza kazi na wengine shughuli zao za biashara kuharibiwa katika ghasia hizo.
NIPASHE
 Naibu Katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), John Mnyika, amesema baada ya Rais Jakaya Kikwete kukabidhiwa ripoti ya uchunguzi wa uchotaji wa fedha za akaunti ya Tegeta Escrow, achukue hatua ya kuwakamata na kuwafilisi watuhumiwa hao.
Aidha, alisema watuhumiwa hao baada ya kukamatwa na kufilisiwa mali zao, wanatakiwa kufikishwa mahakamani pamoja na kuamriwa kurejesha fedha zote walizoiba.
Akihutubia wananchi katika mkutano wa hadhara kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Mkendo katika Manispaa ya Musoma mkoani Mara, alisema iwapo hatua hizo hazitachukuliwa hadi Bunge lijalo la bajeti, Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) watawasha moto upya ili kupata majibu ya kina kabla ya kuelekea uchaguzi mkuu.
Mnyika alisema baada ya Rais kupokea ripoti ya Baraza la Mawaziri, taasisi ya kuzuia rushwa (TAKUKURU) na Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma, ni wakati mwafaka ripoti hizo zikawekwa hadharani ili watuhumiwa wote wafikishwe mahakamani baada ya kufilisiwa mali zao.
Katika kikao chetu na sasa mkutano wetu huu tunatoa azimio la pamoja na tunamtaka Rais Kikwete na tunataka watuhumiwa hao wafikishwe mahakamani na mali zao kufilisiwa ili fedha za umma zirejeshwe,” Mnyika.
Mnyika alisema sakata la Tegeta Escrow mwaka huu, halitafunikwa kama walivyofunika mikataba ‘hewa’, hakuna majibu ya tofauti yatakayotolewa na kusukumiana mpira na viongozi wa sekta zingine bila kujali wao ndiyo wasimamizi wakuu.
Alisema kamwe Chadema hawawezi kuwa wasaliti wa Taifa hili kama bendera ya chama hicho yenye rangi ya kuonyesha upendo, hivyo lazima kitapambana hadi tone la mwisho kuona Watanzania wananufaika na rasilimali za nchi zao.
MTANZANIA
Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani mstaafu, Mzee Nassor Moyo, amesema hajutii kufukuzwa uanachama ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na hatarajii kukata rufaa.
Moyo alisema ataendelea kuwa muumini wa Serikali tatu na kudai mamlaka kamili ya Zanzibar hadi mwisho wa maisha yake.
Alisema anaamini kile anachosimamia ndani ya moyo wake, hivyo hakuna chama wala taasisi yoyote yenye uwezo wa kubadilisha kile anachokiamini kusimamia masilahi ya wananchi wa visiwa vya Zanzibar.
“Naamini ninachofanya na kusimamia siyo dhambi wala usaliti kama baadhi ya wanachama wa CCM wanavyoamini, bali napigania uhuru, usawa wa watu na mapambano haya ni endelevu,” alisema.
Moyo ambaye amekuwa mtumishi wa umma ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa muda mrefu, alisema anatambua mambo mengi ambayo yamefanyika, lakini sasa anashangaa kuona vijana wengi wanajifanya wanajua mambo ya CCM kuliko wazee.
Alipoulizwa kuhusu ukweli juu ya tuhuma zinazomkabili, alisema safari ya kupigania haki na usawa katika maisha ya wanadamu haiwezi kukosa vikwazo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Magharibi, Yussuf Mohamed Yussuf, alikiri Moyo kuvuliwa uanachama na Halmashauri Kuu ya Mkoa huo juzi.
Alisema CCM imetumia busara na hekima nyingi kufuatilia mwenendo wa mwanachama huyo kwa miaka minne baada ya kupokea tuhuma mbalimbali za kukiuka maadili ya chama.
Yussuf alisema miongozi mwa makosa makubwa aliyofanya Moyo, ni kusimama katika majukwaa ya Chama cha Wananchi (CUF) na kudai yeye ni muumini wa Serikali tatu, mfuasi wa kudai mamlaka kamili ya Zanzibar na kujiita mjumbe wa CCM katika Kamati ya Maridhiano ambayo chama chenyewe hakikuhusishwa.
MTANZANIA
Ni dhahiri sasa vyama vya Chadema na ACT-Wazalendo vimeanza kuumana jino kwa jino kutokana na kupishana kwenye mikutano ya kisiasa inayoendelea mikoani.
Wakati vyama hivyo vikiendelea kuchuana na kujaza mamia ya wananchi kwenye mikutano yao, viongozi wake wamekuwa wakituhumiana kwa mambo mbalimbali.
Vyama hivyo vimekuwa vikipishana katika kanda tangu vilipoanza ziara za mikoani hivi karibuni. Wakati Naibu Katibu Mkuu wa Chadema-Bara, John Mnyika akiwa mkoani Mtwara, Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe alikuwa mkoani Ruvuma na timu yake.
Baada ya Mnyika kumalizia ziara hiyo, alirejea Dar es Salaam kabla ya kuanza mikutano yake Kanda ya Ziwa, ambako ACT nao walikwenda.
Akiwa mkoani Mwanza mwishoni mwa wiki, Mnyika akihutubia mamia ya wananchi kwenye viwanja vya Furahisha, alisema Chadema haiko tayari kuwakaribisha ACT-Wazalendo kwenye Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
Lakini siku moja baada ya Mnyika kuondoka Mwanza, Zitto na msafara wake nao waliwasili mkoani humo.
Baada ya kuwasili, Zitto alifanya mkutano wa hadhara kwenye viwanja hivyo hivyo na kusema ACT-Wazalendo wamejipanga kurudisha uzalendo.
Baada ya mkutano huo, jana Zitto aliwasili mkoani Mara ambako alifanya mkutano mkubwa wa hadhara.
Alisema kamwe hatorudi nyuma kwa maneno ya watu, kwani safari ya mapambano imeanza.
Zitto alisema hivi sasa kuna kundi la watu waliojivika upinzani dhidi ya ACT-Wazalendo, ambao wamekuwa wakikesha ili waone chama hicho kinapotea katika siasa za nchi hii.
Akizungumza katika mkutano huo kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Mukendo mjini Musoma, Zitto alisema ameamua kuingia kwenye jahazi la ACT, huku akitambua namna ambavyo anapigwa kila aina ya mishale na watu wasiomtakia mema kwenye siasa.
Alisema anashangazwa na madai ya watu hao kueneza kila aina ya propaganda zenye lengo la kukiua chama cha ACT-Wazalendo, ikiwamo kukihusisha na mipango ya kuwaandalia nafasi baadhi ya makada kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili wagombee urais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu, baada ya kutemwa.
“Mimi ndugu yenu nimepigwa mishale mingi kweli ndani na nje – huko nilikotoka, ikafika mahali unajitahidi kueleza kile unachojua, wenzako hawakutaki, mngekuwa ninyi mngefanyaje?
JAMBOLEO
Simanzi zimetawala katika familia ya mtoto Festo Filbert mwenye miaka 11 iliyopo Majohe kwa Ngosoma, Dar es salaam baada ya mtoto huyo kujinyonga kwa kutumia mkanda wa suruali.
Tukio la kujinyonga kwa mtoto huyo aliyekuwa akisoma darasa la nne katika shule ya Msingi Pugu limeacha huzuni kwa majirani na ndugu zake ambao walikuwa karibu na mtoto huyo.
Mtoto huyo alifikia maamuzi hayo juzi katika maeneo hayo ambapo alikutwa chumbani kwake akiwa amejinyonga na mwili wake ukiwa umeng’inia kwenye mkanda alioufunga shingoni.
Baadhi ya wananchi waliokuwa wakiishi karibu na mtoto huyo walisema wameshtushwa na kifo chake kwani  kabla ya kufikia uamuzi huo alionekana akicheza na wenzake.
Walisema jumapili asubuhi alikwenda kanisani, na aliporudi alikuwa akichezana wenzake lakini walishangazwa na taarifa za kwamba amefariki baada ya kuamua kujinyonga.
Hata hivyo haikuwa rahisi kufahamu sababu za kuamua kujinyonga na sasa maiti yake imehifadhiwa katika hospitali ya Amana huku upelelezi wa Polisi ukiendelea

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...