01 January, 2016

Sasa wezi wa simu wapatikana, wataanza kujiibia wenyewe bila kujijua.


WEZI wa simu nchini watakuwa na wakati mgumu baada ya programu maalumu kubuniwa. Programu hiyo inaweza kulinda taarifa zote za simu ya mteja pamoja na simu yenyewe pindi ikiibwa, ambapo mwizi ataweza hadi kupigwa picha bila mwenyewe kutambua. 
Programu hiyo iliyobuniwa na Mtafiti wa kitanzania, Godfrey Magila kupitia Kampuni yake ya Magila Technologies, itakuwa ikitumiwa na kampuni ya simu za mkononi ya Tigo Tanzania. “Programu hii ni maalumu kwa wateja wa kampuni ya simu za mkononi ya Tigo na inajulikana kama ‘Tigo backup’. 
Imeshaanza kutumiwa na wateja wa kampuni hiyo,” alisema Magila. Magila alisema kuwa wateja wa Tigo, wanaweza kujiunga na programu hiyo ya ulinzi wa taarifa zao zote za simu, ikiwa ni pamoja na simu yenyewe, ambapo simu ikiibwa pia inaweza kupatikana kwa haraka. 
Alisema mara nyingi watu wamekuwa wakipoteza simu zao na taarifa zote katika simu hizo, ikiwa ni pamoja na namba za simu, picha zao za kumbukumbu na vitu vingine muhimu na simu zenyewe, hivyo alibuni kwa lengo la kuwasaidia watanzania kulinda simu zao. 
Kupitia programu hiyo ya ‘Tigo Backup’, mtu anaweza kupata taarifa zake na simu ikipotea, unaweza kutumiwa taarifa zote mahali ilipo simu yako na picha ya mtu anayeitumia simu hiyo pasipo mwizi kujijua. 
Akizungumzia programu hiyo, Meneja Biashara na Maendeleo wa Dar Development Bussiness Incubator (DTBI), Collin Gumbu alisema ubunifu wa programu hiyo ni wa hali ya juu na una uwezo mkubwa huku akizitaka kampuni za mawasiliano nchini kuwaunga mkono vijana wa Tanzania wanaobuni programu za aina hiyo. 
“Vijana wamekuwa wakifanya utafiti na ubunifu wa programu za aina mbalimbali za simu, ambazo kama kampuni za simu nchini zingeweza kuzinunua zingewasaidia sana vijana wetu na kuweza kujiajiri huku wakiitangaza Tanzania kimataifa katika sekta ya sayansi na teknolojia,” alisema Gumbu. 
Gumbu aliipongeza kampuni ya simu ya Tigo kwa kuchukua programu hiyo na kuomba kampuni nyingine nchini kuiga mfano huo. Akiwasiliasha mada katika se mina ya siku moja, iliyoandaliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kwa wahariri wa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam, Gumbu alisema vikwazo vilivyopo katika baadhi ya kampuni, huwarudisha nyuma vijana walio na nia ya ubunifu. 
Alitaja baadhi ya bidhaa ambazo zilibuniwa na watanzania na sasa zinafanya kazi vizuri na kutoa ajira mbalimbali kwa watanzania kuwa ni pamoja na MaxMalipo. Mbali na programu hiyo ya simu za mkononi, pia Magila amebuni programu ambayo inawawezesha watu wenye ulemavu kushiriki katika upigaji kura. 
Pia programu ya simu ambayo inawawezesha wananchi kusikiliza bunge na kushiriki katika mijadala ya Bunge moja kwa moja na kutoa maoni yao wakati bunge likiendelea.

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...