01 January, 2016

Profesa Ndalichako Atoa Siku 30 Kwa Katibu Mtendaji NACTE Kuvichunguza Vyuo Vyote Nchini Kujua Ubora Wake


Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako ametoa siku 30 kwa Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte), Dk Primus Nkwera kufanya ukaguzi wa vyuo vyote na kumkabidhi ripoti ili kujiridhisha na ubora wa elimu inayotolewa.

Pia, amewataka watendaji wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) kuandaa mitalaa yenye matokeo ya kujenga wanafunzi watakaozalisha kwenye jamii.

Waziri huyo ambaye amewahi kuwa Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa (Necta), alitoa maagizo hayo jana wakati wa ziara yake katika ofisi hizo ikiwa ni siku tano baada ya kuapishwa kuiongoza wizara hiyo.

Alisema anawafahamu vyema watendaji wote wa taasisi hizo na hatavumilia kuona ubora wa elimu ukiendelea kuporomoka nchini.

Aliitaka TET kuhakikisha mtalaa wa KKK (Kusoma, Kuandika na Kuhesabu) kwa darasa la kwanza na la pili unapelekwa shuleni kabla ya Januari 13.

“Lakini pili, ningependa muanze kutumia walimu wastaafu kwenye uandaaji mitalaa hiyo na ukaguzi uimarike kwa wanafunzi, mnaweza kuwa na mitalaa mizuri lakini ufuatiliaji ukikosekana haitasaidia,” alisema.

Kuhusu ubora wa elimu alisema: “Ningependa uonekane kwa matokeo baada ya kumaliza shule, sihitaji kusikia amefaulu kwa alama ngapi ila amejengewa uwezo gani kichwani,” alisema.

Alisema kasi ya uwajibikaji TET imekuwa ndogo kwani kitabu cha kurasa 16 kinatengenezwa kwa mwaka mmoja. 

“Ninaweza kuja hapa mnipatie nafasi halafu tujipime na nyie tuone, naomba mbadilike nimeona mko nyuma sana ya kasi yangu,” alisema.

Mbali na maagizo hayo, Profesa Ndalichako aliiagiza Nacte kufanya usajili wa vyuo kwa kuzingatia mahitaji ya soko badala ya kusajili holela bila ufuatiliaji kwa kuwa baadhi vinajiendesha kwa ujanja ujanja.

Alisema suala la ubora wa elimu linamkosesha usingizi. Alilitaka baraza hilo kungeongeza kasi ya ushawishi katika uwekezaji wa shule za ufundi badala ya kujikita kwenye upandishaji wa hadhi ya vyuo na kuondoa dhana ya biashara katika sekta ya elimu.

“Lakini pia ningependa wafanyakazi wote mbadilike, tuache kufanya kazi kwa mazoea. Katika upandishaji hadhi ya vyuo, lazima tujiridhishe na mahitaji ya Taifa, pia kwa suala la udahili wa wanafunzi, ningependa vyuo ambavyo havijatambuliwa kwenye mfumo wa Necta viingizwe ili kuondoa udanganyifu wa vyeti wa usajili,” alisema.    

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...