19 August, 2015

Fimbo ya Lowassa: Wajumbe 32 kumkabili

CCM kimepanga kuzindua kampeni zake za UchaguziChama cha Mapinduzi (CCM) kimetangaza Kamati ya Kampeni yenye wajumbe 32, wengi wao wakiwa ni wale waliowahi kuvaana na mgombea wa Chadema, Edward Lowassa katika masuala tofauti.
Lowassa, Waziri Mkuu wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Nne, alijiondoa CCM mwishoni mwa mwezi uliopita na kujiunga na Chadema, ambayo ilimpa fursa ya kutimiza ndoto yake ya kugombea urais, akiwakilisha vyama vinne vya Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD.
Tangu ahamie Chadema, Lowassa amekuwa akivuta wafuasi wengi kwenye shughuli za Ukawa, hali inayoashiria uwezekano wa kuwapo kwa upinzani mkubwa kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
Jana katika taarifa yake, CCM haikutoa maelezo mengi kuhusu kamati hiyo zaidi ya kutangaza kuwa itaongozwa na Katibu Mkuu wake, Abdulrahman Kinana na kutaja majina ya wajumbe.
“Hii ni kamati ambayo itakuwa inafanya oparations za kila siku,” alisema Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye wakati akitangaza kamati hiyo jana.
Kinana anajulikana kutokana na kazi aliyoifanya ya kuongoza kampeni kwa mafanikio, akifanikisha ushindi wa marais wawili mwaka 1995, wakati alipoongoza kampeni za Rais Benjamin Mkapa na 2005 wakati Rais Jakaya Kikwete akiingia Ikulu.
Licha ya Nape kutozungumzia majukumu ya kamati hiyo, mmoja wa wajumbe, January Makamba alisema wamejipanga vizuri na mwaka huu watafanya kampeni za kisasa.
“Tumejipanga na namna tunavyojipanga ni siri yetu, ni mambo ya ndani ambayo sisi wenyewe kwenye timu tunayafahamu na hatuwezi kutoa siri hizo kwa kuwa  ndizo silaha za maangamizi. Kwa kifupi tutashinda,” alisema naibu waziri huyo wa Mawasiliano Sayansi na Teknolojia.
Makamba, ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli mkoani Tanga, alisema kampeni za CCM mwaka huu zitakuwa za kisasa zinazoendana na mazingira ya kisiasa ya msimu huu.
“Tumejitayarisha kushinda, juhudi zetu na ari yetu ni kushinda na kampeni zetu zitakuwa za kisasa zaidi,” alisema Makamba.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya CCM, Abdallah Bulembo alitumia mfano wa mpira wa miguu kuelezea ukubwa wa kamati hiyo dhidi ya wapinzani.
“Timu hiyo ya kampeni ni sawa na kuileta Arsenal kuja kucheza na timu ya daraja la tatu. Kwa hiyo katika hali hiyo usiulize matokeo,” alisema Bulembo ambaye alikuwa mdau wa soka kabla ya kuingia kwenye siasa.
Kamati hiyo ina wajumbe ambao walitemwa kwenye mbio za urais ndani ya CCM, wajumbe wa Kamati ya Bunge iliyochunguza sakata la Richmond, wajumbe ambao walikuwa kambi ya Lowassa alipokuwa kwenye mbio za urais ndani ya chama hicho, wajumbe ambao ni maarufu kwa kurusha vijembe dhidi ya wapinzani na wajumbe ambao walishaweka bayana uhasimu wao na mbunge huyo wa Monduli.
Nape alisema Kinana atasaidiwa na makamu wenyeviti wawili ambao ni Rajabu Luhwavi (Bara) na Vuai Ali Vuai (Zanzibar) ambao pia ni manaibu wake kwenye chama.
Wajumbe ambao ni wale waliotemwa kwenye mbio za urais ni Dk Asha-Rose Migiro, Samuel Sitta, Mwigulu Nchemba, Dk Harrison Mwakyembe, Makamba, Lazaro Nyalandu, Stephen Wasira, Bernard Membe na Makongoro Nyerere.
Pamoja na kutopitishwa kuwania urais kwa tiketi ya CCM, makada hao wamekuwa wakieleza kuwa hawawezi kuhama chama kama alivyofanya Lowassa na watakuwa wakionyesha kuwa wamevunja makundi kwa kushiriki kumpigia kampeni Dk Magufuli.
Kamati hiyo pia inamjumuisha Sitta, Spika wa Bunge la Tisa ambaye anajulikana kwa kuruhusu mijadala dhidi ya Serikali. Katika mijadala hiyo, Bunge lliliunda kamati iliyoongozwa na Dk Mwakyembe kuchunguza sakata la Richmond lililosababisha Lowassa ajiuzulu uwaziri mkuu.
Katika hotuba yake ya kujiuzulu, Lowassa alidai kuwa suala hilo lilipikwa na mahasimu wake wa kisiasa kwa sababu ya uwaziri mkuu.
Kundi jingine la wajumbe wa kamati hiyo linahusisha makada waliokuwa kambi ya Lowassa alipokuwa anawania urais kupitia CCM lakini hawakuhama naye. Wajumbe hao ni Christopher ole Sendeka, Sadifa Juma Khamis, Shamsi Vuai Nahodha na Sofia Simba, ambaye alipinga uamuzi wa Kamati Kuu wa kupitisha majina matano na kuacha mengine kinyume na katiba.
Wajumbe wengine ni Livingstone Lusinde, Abdallah Bulembo na Nape, ambao wanajulikana kwa kushambulia wapinzani. Lusinde alijipatia umaarufu katika uchaguzi mdogo Jimbo la Arumeru Mashariki, Machi 2012 alipoamua kutumia lugha chafu dhidi ya viongozi wakuu wa Chadema.
Tayari Kinana, Mwigulu, Nape, Bulembo na Wasira wameshanukuliwa wakirusha mashambulizi makali dhidi ya Lowassa na wote waliohama CCM kuwa ni makapi na mafuta machafu na kwamba Magufuli atashinda.
Vilevile, wamo makada waliowahi kutangaza hadharani kuwa mahasimu wa Lowassa tangu alipokuwa ndani ya CCM, akiwamo Anthony Diallo. Kundi jingine ni la makada vijana kama Ummy Mwalimu, Steven Masele na Pindi Chana.
Wakizungumzia uteuzi huo, baadhi ya wajumbe waliishukuru CCM kwa kuwaweka kwenye kamati hiyo huku wakitamba kwamba watahakikisha chama hicho kinaendelea kuongoza nchi.
Mwalimu ambaye pia ni Naibu Waziri wa Sheria na Katiba, alisema uteuzi wake ni jambo linaloonyesha kuwa anaaminika na kuahidi kufanya kazi kwa juhudi kuhakikisha CCM inashinda.
“Kamati imejipanga,” alisema. “Kazi kubwa ni kuhakikisha Dk Magufuli anashinda na anaingia Ikulu kwa kuwa anauzika.
“Hatutishiwi na kitu, tunaamini katika kushinda na kazi yetu kubwa ni kuhakikisha tunashinda kwa kupambana. Magufuli anauzika.”
Ahadi ya kufanya kazi kwa bidii pia ilitolewa na Mbunge wa Kiembesamaki, Waride Bakari Jabu ambaye alisema atajituma kwa asilimia 100 kuhakikisha CCM inashinda.
“Nimefurahi na nitafanya kazi kwa nguvu zangu zote kuhakikisha kuwa tunashika dola Zanzibar na Bara,” alisema.
Wakati Jabu akiyasema hayo, Mbunge wa Viti Maalumu, Dk Maua Daftari alitaka wananchi wawaunge mkono katika kazi hiyo.
“Hili jukumu si la kwanza, lakini ninachoweza kusema ni kuwa wananchi watuunge mkono ili tushinde,” alisema na kusisitiza kuwa watahakikisha kampeni zinafanyika kwa usalama na wala si kwa fujo.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza, Anthony Dialo alisema amepokea uteuzi huo na anachosubiri ni kukaa na kupanga kitakachofanyika.
Makongoro, ambaye ni Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (Eala), alisema hajapata taarifa rasmi kuhusu kuteuliwa kwake kwenye kamati hiyo.
Hata hivyo, alisema hiyo itakuwa ni mara yake ya pili kuwa kwenye kamati ya kampeni kwani aliwahi kufanya kazi kama hiyo alipokuwa NCCR-Mageuzi mwaka 1995. Alisema atazungumza zaidi kuhusu wajibu huo aliopewa pindi atakapopewa taarifa rasmi na Nape.
Wakati Diallo na Makongoro wakisubiri kikao, Nchemba, ambaye ni Naibu Waziri wa Fedha, alitumia nafasi hiyo kumsifu Dk Magufuli.
“Sisi tunachokifanya ni kuweka njia tu ya kwa nini achaguliwe, kuwaambia Watanzania kwa nini anafaa, kwa kuwa awamu ya tano ni awamu ya kazi tu,” alisema.

....MWANANCHI

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...