28 September, 2016

Chuo Kikuu cha Oxford chaongoza ubora wa vyuo vikuu duniani

CHUO kikongwe zaidi katika ulimwengu wa nchi zinazozungumza Kiingereza na kilichotoa viongozi mashuhuri nchini Uingereza cha Oxford, kwa mara ya kwanza kimeongoza katika orodha ya vyuo vikuu duniani, lakini Makamu Mkuu wa chuo hicho ameonya kwamba Brexit inaweza kuharibu mategemeo yake ya muda mrefu.
 
Chuo hicho cha Oxford kimepiku chuo kilichokuwa kikiongoza orodha hiyo kwa miaka mitano iliyopita, cha California Institute of Technology,  ambacho kimeshika nafasi ya pili. Pia orodha hiyo imeshuhudia vyuo vikuu vya China vikipanda kwa haraka zaidi katika orodha hiyo ya vyuo vikuu bora duniani. 

Oxford, walikosoma mawaziri wakuu wane kati ya sita waliopita wa nchi hiyo, kimepiku chuo cha Marekani baada ya bajeti yake ya utafiti kuongezeka kufikia paundi bilioni 1.4 ($1.83bn), wakati matokeo ya utafiti wake ukiongezeka, anasema Phil Baty, mhariri wa orodha hiyo. 

Lakini Baty anasema kujitoa kwa Uingereza kutoka katika Jumuiya ya Ulaya “ni hatari kubwa kwa mafanikio yetu” kwa kufanya kuwa vigumu zaidi kuwavutia wanataaluma wa juu zaidi na kuwaweka katika miradi ya utafiti. 

Brexit inahatari ya kuwaondoa wanafunzi, wafanyakazi na fedha, Makamu Mkuu wa Oxford, Profesa Louise Richardson, aliiambia redio ya BBC. 

Richardson alisema kuwa vyuo vikuu vingine vimeongeza jitihada zake katika kuchukua asilimia 17 ya wafanyakazi wake ambao ni wananchi wa Jumuiya ya Ulaya, na ambao hadhi yao katika Uingereza haiwezi kuhakikiwa baada ya kura ya Juni 23. 

“Vipo vyuo vikuu vingi duniani ambavyo vitafurahi kuwa nao na vimekuwa vikijaribu kuwafuata ili kuwachukua na kuwauliza kama wanaweza kujiunga na vyuo vyao badala ya kuendelea kubaki,” alisema.
Serikali pia imeshindwa kutoa uhakika kama itafidia kiasi cha paundi milioni 67 kwa mwaka ambazo chuo hicho kimekuwa kikipokea kutoka kwa Baraza la Utafiti la Ulaya ambazo hutumika kufanya kazi za utafiti, alisema. 

“Kusema ukweli, tuna wasiwasi juu ya hilo.”
Wakati Oxford, University of Cambridge na London’s Imperial College vya Uingereza vikiwa ndani ya vyuo kumi bora duniani pamoja na chuo kikuu cha ETH Zurich, orodha hiyo imetawaliwa na vyuo vikuu vya kutoka nchini Marekani. 

Chuo Kikuu cha Stanford cha Marekani kimeshika nafasi ya tatu, wakati Massachusetts Institute of Technology, MIT kikishika nafasi ya tano, Havard nafasi ya sita, Princeton saba na Chuo Kikuu cha California, Berkeley na Chuo Kikuu cha Chicago vikifungana katika nafasi ya kumi. Vyote hivi vinatokea nchini Marekani. 

Cambridge cha Uingereza kimeshika nafasi ya nne, wakati Imperial College kikiwa cha nane na ETH Zurich nafasi ya 9.

Chuo Kikuu cha St. Andrews cha Scotland na Chuo Kikuu cha Sheffield vimeporomoka kutoka vyuo vikuu 100 bora duniani. 

Katika Ulaya, nchi za Ujerumani na Uholanzi zimeshika nafasi ya tatu na nne, ambapo Ujerumani ina vyo vipatavyo 41 katika vyo vikuu 200 bora na Uholanzi ikiwa na vyuo vikuu 13 katika orodha hiyo. 

Nchi za Ulaya Kusini kama Hispania na Italia hazijafanya vizuri kutokana na uhaba wa fedha na matatizo katika kuwapata wafanyakazi bora, Baty alisema.

Kwa upana zaidi, orodha inaonyesha taasisi katika bara ya Asia zimepiga hatua, kukiwa na vyuo viwili kutoka barani humo – Chinese University of Hong Kong na Korea Advanced Intitute of Science and Technology – vikiwa ndani ya vyuo 100 bora na vingine vinne vikiingia katika vyuo bora 200. 


Peking University kimepanda hadi nafasi ya 29 kutoka 42, na Tsinghua kikishika nafasi ya 35, kutoka nafasi ya 47 ya mwaka 2015. 

Vyuo vya Asia vinapanda, alisema Baty, wakati serikali ya China ikiingiza mabilioni ya dola katika vyuo vyake wakati huo huo, nchi za magharibi zikikabiliwa na uhaba ya bajeti. 

 Source: RAIA MWEMA

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...