12 May, 2015

KAMA HAUKUPATA CHANCE YAKUPITIA MAGAZETI YA LEO MAY12,2015 JUMANEE HAYA HAPA

NEWSHABARILEO
Mkazi wa kata ya Kisalala, Sumbawanga Lydia Shazi mwenye umri wa miaka 29 amejifungua watoto watatu wote wa kiume kwa siku tofauti katika hospitali mbili tofauti.
Mama huyo ambaye sasa amekuwa na idadi ya watoto saba alieleza kuwa mtoto wake wa
kwanza alijifungulia katika Kituo cha Afya kilichopo mji mdogo wa Laela wilayani Sumbawanga uliopo umbali wa kilometa 97 kutoka mjini Sumbawanga.
Aliongeza kueleza kuwa mtoto huyo alizaliwa Mei 6 mwaka huu katika zahanati hiyo akiwa na uzito wa kilo 2 na gramu 200.
“Wakunga na wauguzi katika kituo cha afya cha Laela walifahamu kuwa nitajifungua mapacha hivyo baada ya kubaini kuwa nina upungufu wa damu mwilini waliamua kunikimbikiza katika Hospitali ya Mkoa wa Rukwa mjini Sumbawanga kwa uchunguzi na matibabu,” .
Aliongeza kuwa alifika hospitalini hapo Mei 6, mwaka huu ambapo alilazwa  “baada ya siku mbili tangu nijifungue mwanangu wa kwanza nilihisi uchungu na nikajifungua mtoto wa pili na watatu Mei 8 , mwaka huu.
“Mtoto wa pili alizaliwa akiwa na uzito wa kilo mbili kamili wakati wa tatu alikuwa na kilo 2 na gramu 600… hawa wawili nilijifungulia hapa hospitali ya mkoa Mei 8, mwaka huu wakati wa kwanza alizaliwa katika kituo cha afya Laela Mei 6, mwaka huu… namshukuru Mungu wanangu wote ni wazima wenye afya njema isitoshe nilijifungua salama tena kwa njia ya kawaida,” alibainisha mzazi huyo.
Akizungumza na gazeti hili hospitalini hapo ambapo mzazi huyo anaendelea kupatiwa matibabu kutokana na kubainika kitabibu kuwa ana upungufu wa damu, ameiomba Serikali na jamii imsaidie chakula na mavazi kwa ajili ya watoto hao kwa kuwa uwezo wake wa kipato kuwahudumia ni mdogo.
“Namshukuru Mungu nimeweza kujifungua salama …licha ya watoto hawa watatu niliojifungua hospitalini hapa, bado nina watoto wengine wanne nyumbani …hali ya kipato mie na mume wangu si nzuri hata kidogo …hivyo naiomba Serikali na jamii inisaidie katika malezi na makuzi ya watoto hawa watatu,” alisisitiza.
Mama huyo alikiri alikuwa akifahamu kuwa angejifungua pacha, lakini hakudhani wangekuwa watoto watatu, “maandalizi yangu kabla ya kujifungua yalikuwa hafifu sana naomba mwenye nguo, mafuta ya kupaka watoto wanisaidie,” alieleza kwa hisia.
Mkunga na muuguzi wa zamu katika wodi ya wazazi hospitalini hapo, Cremensia Kagoma alithibitisha kuwa hali ya kiafya ya mama huyo inazidi kuimarika mara baada ya kupatiwa matibabu ikiwa ni pamoja na kuongezewa damu.
Kwa mujibu wa muuguzi huyo wa zamu, alieleza kuwa mzazi huyo alifika hospitalini hapo hali yake ikiwa duni sana hivyo iliwalazimu wahudumu wa afya hospitalini hapo kuchanga kiasi cha Sh 70,000 ambazo zimetumika kuwanunulia watoto hao nguo nzito ili kuwakinga na baridi..
NIPASHE
Kampuni ya majisafi na majitaka Dar es salaam DAWASCO imetangaza zawadi ya 500,000 kwa yeyote atakayefanikiwa kufichua wezi wa maji katika maeneo yanayopita mabomba ya maji nchini.
 Mtendaji wa DAWASCO Cyprian Luhemela alisema Serikali imejipanga kushirikiana na wananchi na vyombo vya ulinzi likiwemo jeshi la Polisi kudhibiti hali hiyo inayoshamiri kila siku.
Alisema kumekuwepo na upoteaji mkubwa wa maji na kufanya wananchi wengi kukosa maji huku wachache wakinufaika.
Aliwahakikishia wananchi watakaotoa taarifa kwa DAWASCO kuhusu wizi wa maji kwamba zitakuwa siri kati ya mtoa taarifa na mpokeaji ili kulinda usalama wao.
Walisema kwa sasa wameamua kubadilisha sharia badala ya kuwashtaki wezi wa maji kwa kutumia sharia za kawaida sasa watawashtaki kama wahujumu uchumi.
MTANZANIA
Idadi ya watu waliofariki dunia kutokana na athari za mvua na mafuriko Dar es Salaam imeongezeka kutoka wanane na kufikia 12.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema jana kuwa kati ya watu hao mwanaume mmoja anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 35-38, mwili wake ulipoolewa baada ya kuzama kwenye tope katika mto Msimbazi, Magomeni.
Alisema mwili huo wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa ajili ya uchunguzi na utambuzi.
Kamanda aliyataja majina ya watu wengine waliofariki dunia kuwa ni Valerians Eradius (13) ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Kigogo ambaye alikufa Mei 10 mwaka huu baada ya kuangukiwa na ukuta.
Mwingine ni Gervas Shayo (28) mkazi wa Mbezi juu ambaye alikufa maji Mei 8 mwaka huu pamoja na mwanamke mmoja anayekadriwa kuwa na umri kati ya miaka 40 na 45 ambaye jina lake halikufahamika ambaye alikutwa katika bonde la Mkwajuni akiwa amefariki dunia.
Uzoefu unaonyesha kuwa jinsi maji yanavyoendelea kupungua kutokana na kupungua kwa mvua ndivyo madhara yanaonekana.
“Ninawaomba wananchi waendelee kutoa taarifa mapema wanapoona mwili wa mtu aliyekufa ili hatua zichukuliwe mara moja ikiwa ni pamoja na kuiondoa miili ya watu watakaokuwa wamekufa kutokana na athari za mvua inayoendelea kunyesha Dar es Salaam,” Kova.
MWANANCHI
Kada wa CCM Buni Ramole, amejipalia mkaa kutokana na kauli yake kwamba helikopta ya Mbunge wa Moshi Mjini (CHADEMA), Philemon Ndesamburo ni mbovu na ingeweza kumuua.
Ndesamburo kupitia kampuni ya mawakili ya Materu, amemtaka kada huyo kumlipa fidia ya Sh100 milioni na kumwomba radhi, akieleza kuwa kauli hiyo imemdhalilisha na kumvurugia biashara.
Kada huyo wa CCM, anadaiwa kukodi helikopta hiyo Aprili 18, mwaka huu na kwenda nayo katika mkutano wa hadhara wa chama hicho tawala uliofanyika katika viwanja vya Pasua mjini Moshi.
Hata hivyo, baada ya gazeti hili kuripoti tukio hilo, kada huyo alijitokeza hadharani na kukanusha kwamba helikopta hiyo hakuikodi kwa Ndesamburo bali kwa kampuni ya General Aviation Services (T) Limited.
Akizungumza na wanahabari katika ofisi za CCM wilaya ya Moshi Mjini, kada huyo alienda mbali na kudai kuwa helikopta hiyo aliyokuwa aitumie wakati wa kampeni Oktoba mwaka huu, ni mbovu na ingeweza kumuua.
“Nimechukua (chopa) makusudi ili kuwaonyesha wananchi kuwa Chopa si maendeleo. Watu wa Moshi wanafikiri Chopa ni maendeleo, Chopa kazi yake ni kuvuta watu na nimeshaiagiza itakuja, hii niliyokodisha awali ni mbovu kwanza ingeweza kuniua,” .
Hata hivyo, Ndesamburo kupitia mawakili wake hao, amemwandikia barua kada huyo akimtaka akanushe madai hayo, kwani ni ya kashfa na yanaathiri vibaya biashara yake ya Chopa.
”Kwa barua hii tunakutaka ndani ya siku saba, utangaze kwenye gazeti la Mwananchi kwamba taarifa yako ilikuwa si ya kweli na uombe radhi kwa mteja wetu na kumlipa fidia ya Sh100 Milioni,”imedai barua hiyo iliyoandikwa Mei 6 mwaka huu.
Mawakili hao wamedai kuwa wanayo maagizo ya kumfikisha kada huyo mahakamani kama hatatimiza masharti hayo na Ndesamburo atadai fidia kubwa zaidi ya Sh100 Milioni anazodai.
MWANANCHI
Siku moja baada ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad kutoa tuhuma nzito dhidi ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), kuandikisha wapigakura wasio na sifa, tume hiyo imeibuka na kukanusha vikali.
Mkurugenzi wa ZEC, Salum Kassim Ali alisema jana kuwa hakuna majina ya marehemu yanayoendelea kutumika katika Daftari la Kudumu la Wapigakura hivyo CUF iache kuipotosha jamii.
Alikuwa anajibu madai ya Maalim Seif kuwa ZEC iliandikisha na kuruhusu wapigakura wenye umri chini ya miaka 18, walioandikishwa mara mbili, wasiokuwa wakazi na waliotumia ama majina au picha za watu wengine.
Seif ambaye pia ni Katibu Mkuu wa CUF, alisema madai hayo yamebainika katika utafiti uliofanywa na chama hicho ili kubaini hujuma zilizofanywa na SMZ na taasisi zake ambazo zinaweza kufanyika pia katika uchaguzi ujao.
Katika majibu yake, Ali alisema sheria na taratibu za uchaguzi kabla ya kupiga kura, yaani daftari huhakikiwa na majina kubandikwa hadharani katika vituo vya kupigia kura zilifanyika, hivyo kama kungekuwa na dosari, zilipaswa kuwekewa pingamizi.
Alisema sekretarieti ya ZEC inafanya kazi zake kwa maelekezo ya makamishna wake wakiwamo wawili kutoka CUF ambao wanafanya nao kazi kwa ushirikiano mkubwa na hayakuwahi kujitokeza malalamiko hayo.
Alisema kabla ya kuanza uandikishaji mwezi huu, ZEC ilikutana na wadau vyama vya siasa na kuwaeleza mambo manne yatakayofanyika ambayo ni uandikishwaji wa mwisho kwa wapiga kura, kuhakiki daftari la wapigakura, ikiwamo kuondoa waliokufa, kubadilisha taarifa na kuhamisha taarifa za wapigakura.
Alisema endapo kungekuwa na kasoro, makamishna hao wa CUF ndiyo wangekuwa wa mwanzo kulalamika kwa vile wapo jikoni na siyo viongozi wa chama wanaolalamika kwenye vyombo vya habari.
“Kama kweli ana ushahidi wa kile anachokizungumza, kwa nini haleti malalamiko yake ZEC badala yake analalamika kwenye vyombo vya habari?” alihoji.
Mkurugenzi wa Idara ya Usajili wa Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi, Mohamed Juma Ame alisema viongozi wenye dhamana wanapaswa kufanya utafiti na kupata ukweli kabla ya kutoa shutuma nzito ili wananchi wapate taarifa sahihi.
MWANANCHI
Mwili wa mtoto Imran Mwerangi aliyefariki dunia katika Hospitali ya Apollo, India alikokuwa amepelekwa kwa matibabu, unatarajiwa kuwasili leo.
Imran (6), ambaye alipooza mwili mzima na kupata mtindio wa ubongo baada ya kudungwa sindano katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), alifariki dunia saa 11.45 alfajiri ya Mei 8.
Mtoto huyo ambaye alikuwa akipelekwa katika hospitali hiyo, kila baada ya miezi sita kwa ajili ya uchunguzi wa maendeleo ya afya yake kutokana na athari za sindani hiyo, alifikishwa huko Jumatano iliyopita baada ya hali ya afya yake kubadilika na kuvimba mwili mzima.
Alifariki dunia wakati madaktari wakihangaika kupata mishipa ya damu kwa ajili ya vipimo.
Baba wa marehemu, Iddy Mwerangi alisema jana kuwa taratibu za kuurudisha mwili wa marehemu kwa ajili ya mazishi zimefanywa na Ubalozi wa Tanzania nchini India na kwamba mwili huo unatarajiwa kuwasili.
Mwerangi ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), alisema wakati mwili wa marehemu ukitarajiwa kuwasili jioni, mama wa marehemu, Amina Machuro, atawasili mchana. “Baada ya mwili huo kuwasili nchini muda huo, moja kwa moja tutaanza safari kuelekea Mdaula, (Morogoro) kwa ajili ya mazishi,”  Mwerangi.
Imran alidungwa sindano hiyo, Julai 29, 2011 alipopelekwa Muhimbili kwa ajili ya matibabu ya upasuaji mdogo wa nyama zilizokuwa zimeota katika njia ya hewa, puani.
Baada ya kudungwa alitelekezwa ICU bila matibabu kwa zaidi ya miezi sita, akipumua kwa msaada wa mashine, huku ikimlazimu mama yake kumgeuzageuza kila baada ya saa mbili kwa kipindi chote hicho.
Licha ya kutokupata matibabu kwa muda wote huo, juhudi za wazazi wake kuomba rufaa ili apelekwe nje kwa uchunguzi zaidi hazikuzaa matunda hadi gazeti hili lilipoibua taarifa za mkasa wa mtoto huyo Februari 2012 na kuulazimu uongozi wa hospitali hiyo kuunda jopo la madaktari bingwa kuchunguza tukio hilo.
Baada ya ripoti ya uchunguzi huo, ndipo mtoto huyo aliposafirishwa kwenda kutibiwa India.
Aliruhusiwa kurejea nyumbani baada ya madaktari kuridhishwa na maendeleo ya afya yake, akitakiwa kurudi Appolo kila baada ya miezi sita kwa ajili ya uchunguzi.
MWANANCHI
Askofu Mkuu wa Kanisa la General Mission Center Limited (GMCL) la jijini hapa, Nabii David Mpanji juzi alimkabidhi mafuta ya upako, Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba kwa ajili ya kung’arisha nyota yake katika harakati zake za kuwania urais.
Nabii Mpanji alisema mafuta hayo yanaashiria ufalme na utawala na kusisitiza kwamba kitendo hicho ni kudhihirisha kuwa Nchemba, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha, anafaa kuliongoza Taifa.
Tukio hilo lilifanyika kwenye ibada maalumu iliyoambatana na harambee ya kuchangia vifaa vya redio ya kanisa hilo iliyoendeshwa na Nchemba na Sh53 milioni zilipatikana.
Alimtaka Nchemba kutamka nia yake ya kugombea urais mbele za watu, huku akisisitiza kuwa Taifa linahitaji mtu anayeweza kusimamia wananchi wenye kipato cha chini na kumtaja mbunge huyo wa Iramba Magharibi kuwa amethubutu kufanya hivyo.
“Mimi nasema wazee wasikuumize kichwa, hata Biblia inasema fahari ya wazee ni mvi zao lakini fahari ya vijana ni nguvu zao. Tunahitaji Watanzania wazalendo na jasiri ambao wanaweza kusema bila kuogopa kama wewe (Nchemba),” .
Akizungumza katika ibada hiyo, Nchemba aliwashukuru Watanzania wenye imani naye na kubainisha kuwa muda ukifika atasema nia yake.
“Imebaki kitambo kidogo nitasema kwani mimi ni kiongozi wa chama, hivyo natakiwa kufuata taratibu na kanuni cha chama, nawaomba mvute subira kidogo nitasema tu,” alisema.
Nchemba alisema upako huo ni dalili tosha za Watanzania kutambua mchango wake katika kuwatumikia na yeye hatawaangusha… “Tutavuka mto tukifika mtoni.”
Mwigulu ambaye aliongozana na waimbaji maarufu wa nyimbo za Injili akiwamo Boniface Mwaitege na Moses Makondeko, alisema katika suala hilo (la urais) anamtegemea sana Mungu.
Aliwataka wananchi kuwa na uchungu na nchi yao kwa kutanguliza uzalendo kwani ni vigumu kupata kiongozi mzalendo katika Watanzania wasio kuwa na uzalendo.
Akisoma risala mchungaji wa kanisa hilo, Aquina Mhanze alisema mahitaji ya kanisa hilo ni Sh200 milioni kwa ajili ya kukamilisha vifaa vya redio na ofisi na kwamba kwa sasa kuna Sh15 milioni.
Alisema kuwa kati ya fedha hizo, Sh150 milioni ni kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya redio na Sh50 milioni kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya redio.
JAMBOLEO
Serikali iko mbioni kufuta mikataba ya wakandarasi walioshindwa kukamilisha kazi ya kusambaza umeme vijijini kwa wakati uliopangwa.
Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene alisema hayo juzi alipohutubia wananchi wa Kata ya Mlunduzi wilayani Mpwapwa Mkoa wa Dodoma baada ya kukagua miradi ya umeme.
Alisema katika maeneo mengi kazi hiyo imesimama huku wakandarasi wakilipwa fedha nyingi.
“Serikali haiko tayari kucheka na wakandarasi wazembe wanaoshindwa kwenda na kasi inayotakiwa. Natangaza kuanzia leo kuwa tutawafutia mikataba na watarudisha fedha ya umma,” Simbachawene.
Waziri alisema wakandarasi hao wamekuwa wakipoteza muda kwa kuzunguka wakati wote, huku nguzo zikiwa zimelazwa chini na wananchi ndiyo walinzi.
Mkazi wa Mlundizi, Jackson Lengwa alisema wamekuwa wakishangazwa na Serikali kujisifu kuwa umeme unasambazwa wakati wakandarasi hufanya kazi wanapowaona viongozi.
Lengwa alisema kauli ya Waziri Simachawene itakuwa na maana zaidi endapo itatekelezwa kwa vitendo.
Mwakilishi wa Kampuni ya Derm Electricity, Aziz Msuya alisema usambazaji wa umeme wilayani Mpwapwa umefikia asilimia 52 ingawa kwa Mkoa wa Dodoma wamesambaza kwa asilimia 75.
Msuya alisema wanafanya juhudi kubwa kuhakikisha kazi hiyo inakwisha kwa wakati waliokubaliana na Serikali na hawatakubali kukatisha mikataba yao.
MTANZANIA
Kiongozi  wa Uamsho na Jumuiya ya Maimamu Zanzibar, Sheikh Faridi Hadi Ahmed na wenzake 22 wanaokabiliwa na tuhuma za ugaidi wamegoma kula gerezani.
Washtakiwa hao wamegoma kula na wamedai mahakamani kwamba hata waitwe wahaini hawawezi kugeuza madai yao ya kutaka Zanzibar ipate mamlaka yake kamili.
Hayo yalidaiwa jana na washtakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi, Renatus Rutta, wakati kesi yao ilipokuwa inatajwa.
Upande wa Serikali ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Janeth Kitali ulidai upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika hivyo ukaomba kesi iahirishwe huku ukisubiri kumbukumbu za mahakama kwa ajili ya kukata rufaa.
Mshtakiwa Sheikh Farid, alidai chanzo cha kushtakiwa katika kesi hiyo ni madai yao katika mchakato wa katiba ya kuhakikisha Zanzibar inapata mamlaka sahihi.
“Sisi wote ni viongozi wa jumuiya, baada ya yote hayo ndiyo misukosuko ikaanza kwetu, kesi ya ugaidi ni bandia, madai yetu hatuwezi kuyageuza hata watuite wahaini.
“Tulifanyiwa mambo mengi ya ukatili, sisi tunadai heshima ya nchi yetu, tulitamka wazi hatutaki Muungano tunataka Rais wetu apewe heshima yake kama Rais wa Zanzibar,” alidai.
Alidai hawana ajenda ya siri, walifanya mihadhara zaidi ya 200 na walitakiwa kushtakiwa Zanzibar kwa hiyo kutengeneza mazingira hayo ni kutaka kuwadhulumu haki zao.
Sheikh Faridi alidai Serikali iliyopo madarakani imezeeka na ni kikongwe.
MTANZANIA
Hospitali ya Taifa Muhimbili imekumbwa na uhaba mkubwa wa damu hali inayoilazimu uongozi wa hospitali hiyo kuomba msaada wa dharura kutoka kwa Serikali na watu binafsi.
Uongozi huo pia umewaomba Watanzania na watu na Mashirika binafsi kujitokeza kusaidia kuchangia damu ili kuokoa maisha ya wagonjwa katika hospitali hiyo.
Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano na huduma kwa wateja Aminiel Eligaesha alisema kwa siku hospitali hiyo inahitaji chupa za damu 70 hadi 100.
Alisema hali hiyo inachangiwa na ongezeko la mahitaji ya damu ambayo hutumika zaidi hasa kwa wagonjwa wa dharura, kina mama wajawazito, wagonjwa waliofanyiwa upasuaji, watoto na wagonjwa wa saratani

Mawerenewz.blogspot.com ndio mtandao wako wakipekee unaokupa habari za BURUDANI,MICHEZO, SIASA, na HABARI MBALIMBALI ZA KIMATAIFA pamoja na KITAIFA Endelea kutembelea MTOKA MBALI pia nifuate twitter>>>@mawere3, facebook>>>Mawere Mtoka Mbali, Instagram>>>Zawadi_mawere. SuScribe Youtube>>>MAWERE TV.



No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...