04 April, 2015

Jinsi ya Kuishi Maisha Yenye Furaha

Mwanamke akiitazama familia yenye furaha





“Nitakuwa na furaha nikifunga ndoa na kupata watoto.”
“Nitakuwa na furaha nikimiliki nyumba yangu mwenyewe.”
“Nitakuwa na furaha nikipata kazi.”
“Nitakuwa na furaha nikiwa na . . .”
JE, UMEWAHI kuhisi hivyo? Je, ulipopata kile ulichokuwa unatamani, furaha yako ilidumu, au ilianza kupungua? Kwa kweli, kufikia lengo au kupata kitu tulichotamani kunaweza kutufanya tuwe na furaha, lakini furaha hiyo huenda isidumu. Furaha ya kudumu haitegemei tu mafanikio au vitu tulivyo navyo. Badala yake, furaha ya kweli inategemea mambo mengi kama tu jinsi mtu anavyohitaji kufanya mambo mbalimbali ili awe na afya nzuri.
Mahitaji yetu yanatofautiana. Kinachokufurahisha wewe huenda kisimfurahishe mwingine. Kwa kuongezea, tunabadilika tunapoendelea kukua. Ingawa hivyo, uthibitisho unaonyesha kwamba kuna mambo ambayo huhusianishwa na furaha. Kwa mfano, furaha ya kweli inahusiana na kuridhika, kutowaonea wivu wengine, kuwapenda watu, na kutokata tamaa. Acheni tuchunguze mambo hayo.

1. KURIDHIKA

Mwanamume mmoja mwenye hekima alisema hivi: “Pesa ni ulinzi.” Hata hivyo, aliongezea kusema hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili.” (Mhubiri 5:10; 7:12) Alimaanisha nini? Ingawa ni kweli tunahitaji pesa ili kuishi, tunapaswa kuepuka pupa, kwa sababu hatuwezi kutosheleza tamaa hiyo! Mfalme Sulemani wa Israeli la kale, aliyesema maneno hayo, alifanya utafiti ili kuthibitisha ikiwa kuishi maisha ya anasa kunaleta furaha ya kweli. Aliandika hivi: “Sikuyanyima macho yangu chochote ambacho yaliomba. Sikuunyima moyo wangu shangwe ya aina yoyote.”—Mhubiri 1:13; 2:10.
Baada ya kujikusanyia utajiri, Sulemani alijenga majumba makubwa, alitengeneza mabwawa ya kuogelea na bustani maridadi, na alikuwa na wafanyakazi wengi. Alipata kila kitu alichotaka. Alijifunza nini? Mambo hayo yalimletea furaha kwa kiasi fulani, lakini si kwa muda mrefu. Aliandika hivi: “Na, tazama! kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo, wala hapakuwa na lolote lenye faida.” Hata aliyachukia maisha! (Mhubiri 2:11, 17, 18) Kwa kweli, Sulemani alitambua kwamba maisha ya kujistarehesha tu hayaleti furaha ya kudumu. *
Je, utafiti wa kisasa unakubaliana na jambo hilo? Makala moja kwenye Jarida la Masomo ya Jinsi ya Kuwa na Furaha (la Kiingereza) inaeleza hivi: “Mara baada ya mtu kutosheleza mahitaji yake ya msingi, vitu vingine atakavyozidi kupata havitamwongezea furaha.” Kwa kweli, utafiti unaonyesha kwamba ikiwa mtu anaamua kufuatilia maisha ya anasa na kupuuza viwango vya maadili na vya kiroho, anaweza kupoteza furaha.
KANUNI YA BIBLIA: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa.”Waebrania 13:5.

2. EPUKA KUWAONEA WIVU WENGINE

Kamusi moja inafafanua wivu kuwa “uchungu au kinyongo kinachotokana na kutambua kwamba mwingine ana kitu ambacho huna, na pia tamaa ya kutaka kuwa na kitu hicho.” Kama tu uvimbe hatari unaoenea haraka, kuwaonea wivu wengine kunaweza kutawala maisha ya mtu na kumfanya akose furaha. Mtu huanzaje kuwaonea wivu wengine? Tunawezaje kutambua kama tuna tatizo hilo? Na tunawezaje kukabiliana nalo?
Kulingana na kitabu Encyclopedia of Social Psychology watu huwa na mwelekeo wa kuwaonea wivu watu ambao wanalingana nao, huenda katika umri, uzoefu, au malezi. Kwa mfano, si rahisi kwa mfanyabiashara kumwonea wivu mwigizaji maarufu. Lakini huenda akamwonea wivu mfanyabiashara mwenzake mwenye mafanikio kuliko yeye.
Mfano: Maofisa fulani katika utawala wa zamani wa Uajemi, hawakumwonea wivu mfalme, badala yake walimwonea wivu Danieli ofisa mwenzao. Kwa sababu ya wivu wao hata walifanya mpango wa kumwua Danieli! Hata hivyo mpango huo haukufanikiwa. (Danieli 6:1-24) Kitabu Encyclopedia of  Social Psychology kinaendelea kusema hivi: “Ni muhimu tutambue kwamba wivu unaweza kutufanya tutake kuwadhuru wengine. Ndiyo maana kuna visa vingi vya ukatili katika historia ya wanadamu ambavyo vimesababishwa na kuwaonea wivu wengine.” *

3. WAPENDE WATU

Kitabu Social Psychology kinasema: “Ikiwa watu wana uhusiano mzuri miongoni mwao, jambo hilo linaweza kuwafanya wafurahie maisha hata kuliko furaha inayopatikana kwa kuwa na kazi, mshahara mnono, kukubaliwa katika jamii, au kuwa na afya nzuri.” Kwa ufupi, ili wanadamu wawe na furaha ya kweli, wanahitaji kupenda na kupendwa. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema hivi: “Ikiwa . . . sina upendo, mimi si kitu.”—1 Wakorintho 13:2.
Sisi sote tuna nafasi ya kusitawisha upendo. Kwa mfano, Vanessa alikuwa na baba mkatili na mlevi kupindukia. Alipokuwa na umri wa miaka 14, alitoroka nyumbani na hakuwa na makazi maalumu, na hata alimwomba Mungu amsaidie. Kisha, inaonekana kwamba Mungu alimsaidia kwa sababu alianza kuishi na familia iliyofuata kanuni ya Biblia inayosema “upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili.” (1 Wakorintho 13:4) Kuishi na familia hiyo na kujifunza Biblia, kulimsaidia Vanessa kupona kihisia na kiakili. Alisema hivi: “Nilianza kufaulu masomoni na alama zangu zikawa bora.”
Vanessa bado anakumbuka mambo yaliyompata zamani. Hata hivyo, sasa ana ndoa yenye furaha na ni mama wa wasichana wawili.
KANUNI YA BIBLIA: “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”Wakolosai 3:14.

No comments:

Post a Comment

Samsung kurejesha fedha kwa wanunuzi wa Note 7

KAMPUNI ya Vifaa vya Elektoriniki ya Samsung ya Afrika Mashariki (SEEA) itarejesha fedha kwa wateja wa simu za Note 7, ambao wataweza kuthib...